Wasira: 'Mitano tena' ni kwa Rais Samia, wengine watasubiri mchujo

 

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, amesema kaulimbiu ya "Mitano Tena" ni kwa ajili ya mgombea urais wa chama hicho Dk. Samia Suluhu Hassan na mgombea mwenza wake Dk. Emmanuel Nchimbi pekee, huku akiweka wazi kuwa wabunge na madiwani hawajapewa uhakika bali watapitia mchujo wa ndani ya chama.

Wasira ameyasema hayo leo Juni 11, 2025, alipokuwa akizungumza katika kikao cha ndani na viongozi wa CCM wa Wilaya ya Nyasa, kilichofanyika katika mji wa Mbamba Bay mkoani Ruvuma, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kuimarisha Chama.

“Niwaambie wana CCM wenzangu, tunaposema Mitano Tena ni kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na mgombea mwenza wake Dk. Emmanuel Nchimbi. Kwa wabunge na madiwani tusubiri mchujo ndani ya Chama,” alisema Wasira huku akisisitiza kuwa mchujo huo utafanyika kwa haki na kwa kuzingatia maoni ya wananchi.

Ameongeza kuwa mwaka huu CCM imeongeza idadi ya wapigakura wa maoni katika maeneo mbalimbali nchini ili kuhakikisha mchakato wa kupata wagombea unakuwa shirikishi zaidi.

“Kwa mfano hapa Nyasa, mwaka uliopita walikuwa wapigakura 900, sasa hivi wako 1,300. Hii ni ishara ya kupanua demokrasia ndani ya Chama,” alifafanua.

Wasira amesisitiza kuwa si kila kiongozi aliyepo madarakani atapewa fursa ya kurejea moja kwa moja, bali ni wananchi kupitia kura za maoni ndio watakaoamua nani anafaa kuendelea.

“Sio kila mtu ni Mitano Tena, bali ni kwa Rais Samia. Wengine tutachujana. Mbunge au diwani anayetaka kuendelea, anatakiwa akubali kupimwa na wapigakura wa kata yake,” alieleza.

Katika kikao hicho, alionya dhidi ya wagombea wanaotafuta uongozi kwa kutumia fedha kununua kura, akisema chama kinataka watu safi na wanaokubalika mbele ya wananchi.

“Mabalozi wa CCM wana jukumu la kuhakikisha wanapitisha majina ya wagombea ambao wanauzika kwa wananchi, si wale waliopita kwa hela. Heshima ya mjumbe ni kusikiliza sauti ya waliomchagua,” alisema.

Katika ziara hiyo, Wasira pia alikagua maendeleo ya ujenzi wa Bandari ya Mbamba Bay, wilayani Nyasa, mradi ambao Serikali imewekeza fedha kwa ajili ya kuuboresha na kuimarisha miundombinu ya usafirishaji katika Ukanda wa Ziwa Nyasa.




Chapisha Maoni

0 Maoni