Utalii wazidi kuing'arisha Tanzania, mapato yafikia dola bilioni 3.9

Sekta ya utalii nchini Tanzania imeendelea kushuhudia mafanikio makubwa, kufuatia mikakati ya Serikali katika kuimarisha na kutangaza vivutio vya utalii kimataifa. 

Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa bungeni leo Jijini Dodoma na Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba, imesema idadi ya watalii wa kimataifa imeongezeka kutoka 1,183,416 mwaka 2020 hadi 5,360,247 mwaka 2024. 

Dkt. Nchemba, amesema mapato yatokanayo na sekta hiyo pia yamepanda kutoka dola za Marekani milioni 715 mwaka 2020 hadi dola bilioni 3.9 mwaka huu, hali iliyoifanya Tanzania kutambulika kuwa miongoni mwa nchi tatu bora barani Afrika kwa ongezeko la mapato ya utalii. 

Mafanikio hayo yanatajwa kuwa matokeo ya juhudi mahususi zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita, ikiwemo kutengeneza filamu za kimataifa kama Tanzania – The Royal Tour na Amazing Tanzania, ambazo zimetumika kuitangaza nchi na vivutio vyake duniani kote. 

Tanzania pia imetajwa kuwa kinara wa nchi zinazovutia watalii Afrika kwa mwaka 2024 (Africa’s Leading Destination), huku Hifadhi ya Taifa Serengeti ikishinda tena tuzo ya hifadhi bora duniani kwa mwaka wa tano mfululizo.

Waziri wa Fedha Dkt. Nchemba, ameongea hayo leo Jijini Dodoma wakati akiwasilisha Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali, ambapo ameliomba Bunge ridhaa ya kukusanya na kutumia jumla ya shilingi trilioni 56.49 kwa Mwaka wa Fedha 2025/26.

Bajeti hiyo, ambayo ni kubwa zaidi kuwahi kuwasilishwa katika historia ya nchi, inalenga kuendeleza mageuzi ya kiuchumi, kuboresha huduma za kijamii, na kuimarisha sekta zinazochochea maendeleo kama kilimo, viwanda, na utalii. 

Kwa mujibu wa Dkt. Nchemba, mafanikio ya utalii si tu yameongeza mapato ya Serikali bali pia yamefungua fursa mpya za ajira kwa vijana na kuinua kipato cha wananchi katika maeneo yanayozunguka vivutio vya utalii. 

“Tumejipanga kuendeleza mafanikio haya kwa kuwekeza zaidi kwenye miundombinu ya utalii, masoko ya kimataifa, na mafunzo kwa wadau wa sekta hii muhimu,” alisema Waziri wa Fedha Dkt. Nchemba.

Bunge linatarajiwa kujadili bajeti hiyo katika siku zijazo, huku Watanzania wengi wakiwa na matumaini ya kuona utekelezaji wake ukiakisi ahadi ya Serikali ya kuleta maendeleo ya kweli kwa wananchi wote.

Chapisha Maoni

0 Maoni