Deni la Taifa lafikia Tril. 107.70, bado ni himilivu

 

Serikali imesema kuwa hadi kufikia Aprili 2025, deni la taifa limefikia shilingi trilioni 107.70, likiwa bado ndani ya viwango vya uhimilivu, huku ikiahidi kuendelea na mikakati ya kuhakikisha haligeuki mzigo kwa uchumi wa nchi.

Akiwasilisha hotuba ya bajeti kwa mwaka wa fedha 2024/25 bungeni leo, Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kati ya kiasi hicho, deni la nje ni shilingi trilioni 72.94 huku deni la ndani likiwa shilingi trilioni 34.76.

“Mheshimiwa Spika, tathmini ya uhimilivu wa deni iliyofanyika Oktoba 2024 inaonesha kuwa deni la Serikali ni himilivu kwa muda mfupi, wa kati na mrefu,” alisema Dkt. Mwigulu na kuongeza: “Thamani ya sasa ya deni la Serikali kwa Pato la Taifa ni asilimia 40.3, chini ya ukomo wa asilimia 55. Aidha, thamani ya sasa ya deni la nje kwa Pato la Taifa ni asilimia 23.6 dhidi ya ukomo wa asilimia 40, na kwa mauzo ya nje ni asilimia 123.8 huku ukomo ukiwa asilimia 180.”

Katika kuimarisha uaminifu wa Tanzania katika masoko ya fedha ya kimataifa, Dkt. Mwigulu alisema kampuni ya kimataifa ya Moody’s Investors Service ilifanya tathmini Machi 2025 na kuiweka Tanzania katika daraja la B1, sawa na ilivyokuwa mwishoni mwa mwaka 2024.

“Pia, kampuni ya Fitch Ratings inaendelea na mapitio yake ya mwaka 2025 na matokeo yanatarajiwa kutangazwa hivi karibuni. Katika tathmini yake ya mwisho Desemba 2024, Tanzania iliwekwa katika daraja la B+,” alisema.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, nafasi hiyo ya nchi katika madaraja ya kimataifa inaendelea kutoa taswira chanya ya Tanzania kimataifa, ikiwa ni bora kuliko baadhi ya nchi nyingine katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Dkt. Mwigulu alieleza kuwa matokeo hayo yamechangiwa na juhudi za Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kupitia usimamizi madhubuti wa uchumi, uimarishaji wa mazingira ya uwekezaji na ushirikiano wa kimataifa.

Katika kuhakikisha deni linaendelea kuwa himilivu, Serikali imesema itaendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kupunguza utegemezi wa mikopo, kuelekeza fedha za mikopo katika miradi ya kimkakati inayoongeza mapato na mauzo nje ya nchi, na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatayarishwa ipasavyo kabla ya kuingia mikataba.

“Maafisa Masuuli wote wanaelekezwa kuzingatia maandalizi ya miradi kwa mujibu wa sheria, kanuni na miongozo iliyopo ili kuepusha ongezeko la gharama zisizo za lazima,” alisisitiza Waziri huyo.

Waziri wa Fedha, anamewasilisha Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali, ambapo ameliomba Bunge ridhaa ya kukusanya na kutumia jumla ya shilingi trilioni 56.49 kwa Mwaka wa Fedha 2025/26.

Chapisha Maoni

0 Maoni