Rais wa Benki ya
Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayemaliza muda wake, Dkt. Akinwumi Adesina,
amewasili jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Juni 12, 2025 kwa ziara ya kikazi
ya siku nne ambayo itamfikisha katika mikoa mbalimbali nchini.
Mara baada ya
kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dkt.
Adesina alipokelewa na Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe pamoja na Naibu
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Denis Londo.
Katika ratiba ya
ziara yake, Dkt. Adesina anatarajiwa kufanya mazungumzo rasmi na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mazungumzo hayo
yanatarajiwa kugusia maeneo ya ushirikiano baina ya Tanzania na Benki hiyo,
hususan katika sekta ya miundombinu, kilimo na uwezeshaji wa vijana.
Mnamo Juni 14, 2025,
Dkt. Adesina na Rais Samia watashiriki hafla ya uzinduzi wa Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Msalato pamoja na barabara ya mzunguko ya jiji la Dodoma, miradi
ambayo inatekelezwa kwa msaada wa kifedha kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika.
Katika hatua nyingine
ya heshima, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimetangaza kumtunuku Dkt.
Adesina Shahada ya Heshima ya Uzamivu (Falsafa) kwa kutambua mchango wake
mkubwa katika maendeleo ya bara la Afrika, hasa kupitia mageuzi ya kilimo na
uwekezaji katika miradi ya kimkakati. Hafla ya kutunuku shahada hiyo itafanyika
Juni 13, 2025 jijini Dar es Salaam.
Ziara ya Dkt. Adesina
inatazamwa kama fursa ya kuimarisha uhusiano wa Tanzania na taasisi hiyo kubwa
ya kifedha barani Afrika, huku nchi ikiendelea kusaka fursa zaidi za uwekezaji
na ushirikiano wa maendeleo.
0 Maoni