TFS yaleta huduma ya kudungwa na nyuki maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani

 

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeendelea kuwakaribisha wananchi katika banda lake maalum kwenye Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete (JKCC), jijini Dodoma, ambapo pamoja na mambo mengine, unatoa huduma ya tiba ya kudungwa na nyuki (api-therapy) bure kabisa kwa wananchi.

Huduma hiyo ni sehemu ya juhudi za TFS kuwaelimisha Watanzania juu ya manufaa ya uhifadhi wa mazingira kupitia njia za asili. Kwa mujibu wa Mhifadhi Brenda Mwakipesile kutoka Hifadhi ya Mazingira Asilia ya Vikindu, huduma hiyo inalenga kuimarisha kinga ya mwili, kupunguza maumivu ya viungo, kuboresha mzunguko wa damu, na kusaidia afya ya akili.

“Tumeileta huduma hii bure kwa wananchi ili kuwaonesha kuwa uhifadhi wa misitu hauishii kwenye miti pekee, bali pia unaweza kuzaa tiba za asili ambazo ni salama na zenye manufaa ya kiafya,” alisema Mhifadhi Brenda.

Kwa upande wake, Mkuu wa Banda la TFS katika maonesho hayo, Mhifadhi Mkuu Kassim Ally, alisema ushiriki wa taasisi hiyo katika maadhimisho ya mwaka huu unaendana na kaulimbiu ya kitaifa isemayo “Mazingira Yetu na Tanzania Ijayo, Tuwajibike Sasa – Dhibiti Matumizi ya Plastiki.”

“TFS tunashiriki kama wadau wakuu wa uhifadhi, tukionesha namna misitu inavyoweza kutumika kwa njia endelevu, kuanzia elimu ya mazingira, huduma za afya, matumizi ya malisho kwa mifugo, hadi uzalishaji wa miche ya miti,” alisema Ally.

TFS inawahimiza wananchi wote kujitokeza kushiriki katika maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Duniani yanayoendelea hadi Juni 5, 2025, kwa lengo la kujifunza, kufurahia, na kupata huduma za kipekee zitolewazo na wataalamu wa uhifadhi wa misitu. 

Naibu Katibu Mkuu (Muungano), Ofisi ya Makamu wa Rais, Bw. Abdallah Hassan Mitawi, akipatiwa huduma ya tiba ya kudungwa na nyuki (api-therapy) kutoka kwa Mhifadhi Brenda Mwakipesile wa TFS – Hifadhi ya Mazingira Asilia ya Vikindu, katika viwanja vya JKCC, Dodoma. Huduma hiyo inalenga kuimarisha kinga ya mwili kwa kutumia tiba asilia kutoka kwenye mazingira ya misitu, ikiwa ni sehemu ya kuonesha mchango wa uhifadhi katika afya na utalii wa Mazingirq. Huduma hiyo inatolewa bure kwa wananchi wote wanaotembelea banda la TFS.



Chapisha Maoni

0 Maoni