Siku ya Baba Duniani: Walio kimya, wenye kubeba mzigo mkubwa

 

Kila mwaka, Juni 15 dunia huadhimisha Siku ya Baba Duniani. Siku maalum ya kutambua mchango wa baba katika familia na jamii kwa ujumla. Ingawa mara nyingi huonekana kama wanyenyekevu, wasio na makelele, mababa wana nafasi ya kipekee isiyoweza kufunikwa katika maisha ya kila mtoto.

Katika maisha yetu, mara nyingi tunasikia kauli kama “mama ni kila kitu,” na bila shaka mama ana nafasi ya kipekee. Lakini je, tumewahi kutafakari nafasi ya baba? Ni nani aliyekufundisha kuendesha baiskeli, kukata kuni, au kuamini kuwa unaweza kuwa jasiri hata ukiwa umechoka? Baba ndiye nguzo isiyoonekana mara nyingi, lakini inayobeba msingi wa familia.

Baba: Shujaa wa Kimya

Baba anaweza kuwa si msemaji sana, lakini anasema kwa vitendo. Anaamka mapema, anajinyima ili familia ipate. Mara nyingi huziba pengo pasipo kulalamika, anapokosekana meza ya chakula si kwa sababu ya kutojali, bali kwa sababu yuko kazini, anatafuta mkate wa familia.

Baba wa Kisasa: Zaidi ya Mlezi

Enzi zimebadilika. Baba wa sasa si tu mtafutaji wa kipato, bali pia mlezi wa kihisia. Anabadilisha nepi, anahudhuria mikutano ya wazazi shuleni, anasikiliza matatizo ya watoto wake na kuwashauri kwa upendo. Huyu ni baba anayejenga siyo tu nyumba, bali familia yenye maadili, mshikamano na ndoto.

Tuwaenzi Walio Hai, Tukumbuke Waliotangulia

Katika siku hii ya baba, hatuna budi kuwaenzi waliopo kwa neno jema, kwa zawadi ndogo, hata kwa ujumbe mfupi wa shukrani. Kwa waliotangulia mbele ya haki, tuwakumbuke kwa sala na kwa kuenzi mafundisho yao.

Mwisho wa Siku...Baba ni zaidi ya jina. Ni jukumu. Ni moyo wa kujitoa. Ni bega la kutegemewa.

Leo, tuwaambie kwa sauti: Asante Baba. Tunakuthamini. Tunakupenda.

Chapisha Maoni

0 Maoni