Rais Samia: Jaji Mkuu Masaju huko peke yako, nitakuwa msaada wako

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amemhakikishia Jaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania, George Masaju, kuwa hatabaki peke yake katika kutekeleza majukumu ya mhimili huo muhimu wa dola, akiahidi kushirikiana naye kwa karibu katika nyakati zote – hasa anapohitaji msaada.

Rais Samia alitoa kauli hiyo leo Jumapili, Juni 15, 2025, wakati wa hafla ya kumuapisha Jaji Mkuu Masaju iliyofanyika Ikulu, jijini Dodoma.

“Kwa Jaji Mkuu mpya, kwanza nikupongeze na pia nikupe pole, maana mzigo huu si mdogo, una kazi kubwa ya kufanya,” alisema Rais Samia kwa sauti ya matumaini na mshikamano.

Katika kumtia moyo kiongozi huyo wa Mahakama, Rais Samia alitoa mfano wa ndege iliyoko angani inayokaribia kuishiwa mafuta, akisisitiza kuwa ni vyema kusimama kwa muda na kujaza tena nguvu ili safari iendelee.

“Nataka nikupe mfano mmoja tu,” alisema Rais. “Ndege ikiwa angani na mafuta yakikaribia kuisha, haipaswi kulazimisha kutua kwa heshima, bali kutafuta kiwanja cha karibu, jaza mafuta, uruke tena. Na unapohitaji kujaza mafuta hiyo ndege yako, niwe mimi mtumishi wako wa kukuwekea yale mafuta, ili uweze kuruka tena na safari iendelee.”

Kauli hiyo ya Rais Samia imeonekana kugusa wengi waliohudhuria hafla hiyo, ikionesha dhamira yake ya kuimarisha mahusiano kati ya mihimili ya dola, huku akionyesha wazi kuwa yuko tayari kuwa bega kwa bega na Jaji Mkuu katika kusimamia haki na sheria nchini.

George Masaju aliteuliwa kuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania hivi karibuni, akichukua nafasi hiyo muhimu katika kipindi ambacho mfumo wa utoaji haki unaendelea kufanyiwa maboresho mbalimbali chini ya serikali ya awamu ya sita.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Jaji George Mcheche Masaju kuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 15 Juni, 2025.

Picha ya matukio mbalimbali kwenye hafla ya uapisho wa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 15 Juni, 2025.

Chapisha Maoni

0 Maoni