Mambo yote ni Mpanga/Kipengere Siku ya Maporomoko Duniani

 

Hifadhi ya Taifa ya Mpanga/Kipengere, inayopatikana katika mikoa ya Mbeya na Njombe, inajiandaa kuandika historia mpya kwa kuadhimisha Siku ya Maporomoko Duniani kwa kishindo kikubwa, Juni 16 mwaka huu.

Katika maadhimisho hayo, kutakuwa na Nyamapori Festival, sambamba watu kufurahia ladha halisi ya vyakula vya asili vitakavyoandaliwa kwa kuzingatia mila na tamaduni za wakazi wa maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.

Miongoni mwa mambo makubwa yatakayofanyika siku hiyo ni uzinduzi rasmi wa barabara  inayowawezesha watalii kufika kwa urahisi katika eneo la kipekee la bustani ya dunia,  eneo ambalo awali lilikuwa na changamoto ya miundombinu, sasa limefunguliwa rasmi kwa mara ya kwanza.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), barabara hiyo sasa imekamilika na inawawezesha watalii kufika katika eneo hilo lenye kapeti la maua ya aina mbalimbali,  tukio ambalo litakuwa la kwanza kabisa kushuhudiwa na wageni wa ndani na nje ya nchi.

"Hii ni fursa adimu ya kushuhudia mandhari ya kuvutia, yakiwemo maporomoko 58 ya maji ndani ya hifadhi, pamoja na vivutio vingine vingi vya kiasili," imesema sehemu ya taarifa ya TAWA.

Wakazi wa maeneo ya karibu, wageni kutoka sehemu mbalimbali nchini, na hata wageni wa kimataifa, wanahimizwa kujitokeza kushiriki katika tukio hili la kihistoria litakalotoa taswira halisi ya utalii wa ndani unaozingatia mazingira, utamaduni, na uhifadhi endelevu.

Chapisha Maoni

0 Maoni