Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amemtaka Mkurugenzi Mtendaji
mpya wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Delilah Kimambo kuhakikisha
anaendeleza ubora wa huduma na kuimarisha uongozi wa hospitali hiyo kongwe na
ya kimkakati katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Akizungumza leo Juni
28, 2025 katika viwanja vya Ikulu Chamwino mkoani Dodoma wakati wa kuwaapisha
viongozi mbalimbali aliowateua hivi karibuni, Rais Samia amesema Muhimbili
inahitaji uongozi wa kitaalamu na wa kiutawala ili kuendelea kutoa huduma bora
za kibingwa na kuimarisha utalii wa tiba.
“Muhimbili inahitaji
professionalism na administrative skills. Nimepitia wasifu wa watu wengi lakini
nikaona wewe Dkt. Delilah Kimambo ndiyo unafaa kuiongoza hospitali hiyo. Nenda
kaendeleze pale alipoishia Prof. Janabi,” amesema Rais Samia.
Katika hotuba hiyo,
Rais Samia amemwelekeza Dkt. Kimambo kuhakikisha huduma zinazotolewa na
Muhimbili zinaendelea kukidhi viwango vya kimataifa, sambamba na kusimamia
kikamilifu matumizi ya rasilimali zilizowekezwa na Serikali kwa ajili ya
kuboresha hospitali hiyo.
Amesema Serikali
imefanya uwekezaji mkubwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kuimarisha
vifaa tiba vya kisasa na kuleta wataalamu wa juu, ili kuiwezesha hospitali hiyo
kutoa huduma bora kwa Watanzania na wageni wanaokuja kupata matibabu nchini.
Aidha, Rais Samia
amesema tayari Serikali imepata fedha kwa ajili ya maboresho ya zaidi katika
hospitali hiyo, hususan kwenye ujenzi wa miundombinu ya majengo mapya, ikiwa ni
muendelezo wa juhudi za kuboresha sekta ya afya nchini.
Dkt. Delilah Kimambo
aliteuliwa na Rais Samia tarehe 16 Juni, 2025 kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa
Hospitali ya Taifa Muhimbili, kuchukua nafasi ya Prof. Mohamed Janabi ambaye
amehamishiwa katika majukumu mengine ya kitaifa.
Hospitali ya Taifa
Muhimbili ni miongoni mwa taasisi muhimu za tiba nchini na inatajwa kuwa
kiongozi wa huduma za kibingwa na utalii tiba katika Ukanda wa Afrika Mashariki
na Kati.


0 Maoni