NHC kuanza kugawa nyumba 560 Kawe, za Samia Housing Scheme

 

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) linatarajia kuanza kugawa nyumba za makazi 560 kwa wanunuzi wa nyumba za mradi wa Samia Housing Scheme (SHS) uliopo Kawe Jijini  Dar es Salaam baada ya kukamilika kwa mradi huo.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah Hamad amesema katika wiki ya mwisho ya mwezi huu wa Juni, 2025 wataanza kuwagawia wamiliki nyumba 200 zilizokwisha kamilika kati ya nyumba 560 za Samia Housing Scheme Kawe.

“Wiki ya mwisho ya mwezi huu (Juni) tutaanza kuwagawia wamiliki wa Samia Housing Scheme nyumba 200 na hadi kufikia katikati ya Julai tutakuwa tumewakabidhi wamiliki wote nyumba zao katika mradi wa Samia Housing Scheme Kawe awamu ya kwanza,” amesema Bw. Hamad.

Amesema nyumba hizo 560 za Samia Housing Scheme za majengo kumi ya ghorofa yenye ghorofa kumi kila moja zilizojengwa katika eneo la Kawe Jijini Dar es Salaam na kuuzwa zote zimejengwa gharama ya Shilingi bilioni 48.

Bw. Hamad ambaye alikuwa akiongea na wahariri wa vyombo vya habari jana Jijini Dar es Salaam amesema NHC linaendelea na mapango wa ujenzi wa nyumba 5,000 za gharama ya kati chini kupitia mradi wa Samia Housing Scheme ambao utekelezaji wake unaendelea.

Amesema mradi huu wa nyumba za kuuza na kupangisha unakusudia kuenzi kazi nzuri anazofanya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo kuwezesha upatikanaji wa mikopo ya ujenzi wa nyumba bora nchini.

Bw. Hamad amesema Shirika la Nyumba ya Taifa litaendelea na ujenzi wa nyumba 5,000 za Samia Housing Scheme katika maeneo mbalimbali nchini ambayo ameyataja kuwa ni ya Medeli, Mtoni Kijichi, Kawe 711 na Iyumbu.

Ameeleza kuwa asilimia 50 ya nyumba hizo zitajengwa katika Mkoa wa Dar es Salaam, asilimia 20 katika mkoa wa Dodoma na asilimia 30 zitajengwa katika mikoa mingine.

Aidha, Bw. Hamad amesema mradi huu wa nyumba 5,000 unaotekelezwa kwa awamu, utagharimu takriban Shilingi bilioni 466 sawa na dola za Kimarekani milioni 200.

Ameeleza kuwa awamu ya pili ya utekelezaji wa mradi huu imeanza eneo la Medeli, Jijini Dodoma; na Kawe na Kijichi Jijini Dar es Salaam ambapo nyumba 908 zinajengwa. Ujenzi wa nyumba 68 Iyumbu zimekamilika kwa asilimia 100.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Hamad Abdallah Hamad akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari Jijini Dar es Salaam.

Chapisha Maoni

0 Maoni