Mgombea Urais Colombia apigwa risasi kichwani

 

Mgombea urais nchini Colombia, Seneta Miguel Uribe Turbay (39), amelazwa hospitalini akiwa  mahututi baada ya kupigwa risasi mara tatu, ikiwemo mara mbili kichwani akiwa kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika Jumamosi katika bustani moja jijini Bogotá.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, kijana mwenye umri wa miaka 15 alikamatwa katika eneo la tukio na anashikiliwa na polisi kwa mahojiano kuhusiana na shambulio hilo.

Mke wa seneta huyo, Maria Claudia Tarazona, amewaomba wananchi wa Colombia kuungana kwa maombi kwa ajili ya uzima wa mumewe. “Miguel kwa sasa anapigania maisha yake. Tumwombe Mungu awaongoze madaktari wanaomhudumia,” alisema Tarazona kwa uchungu.

Chama chake cha Centro Democrático kimelaani vikali tukio hilo, kikieleza kuwa ni tishio kwa demokrasia na uhuru nchini humo.

Video iliyorekodiwa kwa simu na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii inaonyesha tukio la kupigwa risasi wakati Turbay akiwasilisha hotuba, hali iliyozua taharuki na kusababisha watu kukimbia kwa hofu.

Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, wahudumu wa afya wamesema Turbay alipigwa risasi kwenye goti na mara mbili kichwani. Alipelekwa hospitalini kwa helikopta ambapo wafuasi wake walikusanyika kwa ajili ya sala na dua.

Meya wa Bogotá, Carlos Fernando Galán, amesema Turbay amefanyiwa upasuaji na kwa sasa yuko kwenye saa muhimu za awali za uangalizi akiwa mahututi.

Chapisha Maoni

0 Maoni