Denmark kuimarisha ushirikiano wake na Tanzania

 

Ufalme wa Denmark umeweka wazi dhamira  yake ya kuimarisha ushirikiano wa karibu na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika nyanja za kisiasa, kiuchumi na kidiplomasia, ili kuchochea maendeleo ya pamoja kati ya mataifa hayo mawili.

Hayo yamebainishwa Juni 5, 2025, katika hafla ya maadhimisho ya Siku ya Katiba ya Denmark (Grundlovsdag) iliyofanyika kwenye makazi rasmi ya Balozi wa Denmark nchini, jijini Dar es Salaam. Hafla hiyo ilikuwa ni sehemu ya kumbukizi ya miaka 176 tangu kutiwa saini kwa Katiba ya Denmark mwaka 1849 — moja ya Katiba kongwe zaidi duniani.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Mahmoud Thabit Kombo, ambaye aliongozana na viongozi wa kibalozi, wawakilishi wa sekta binafsi, mashirika ya maendeleo, asasi za kiraia na wanahabari.

Akihutubia wageni waalikwa, Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mheshimiwa Jesper Kammersgaard, alisema kuwa taifa lake limechagua kuendeleza uwepo wake wa kidiplomasia nchini Tanzania kama sehemu ya mwelekeo mpya wa sera ya nje ya Denmark barani Afrika.

“Leo tunasema kwa kauli moja, Denmark imerudi rasmi Tanzania,” alisema Balozi Kammersgaard huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kweli, wa kuaminiana na wenye misingi ya kuheshimiana.

Alibainisha kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kipindi cha miaka 15 iliyopita, hasa katika ukuaji wa tabaka la kati na maendeleo ya sekta za kilimo na biashara. Vilevile, aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa mwelekeo wake mpya wa sera za kigeni, hasa diplomasia ya kiuchumi inayotoa nafasi kwa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Waziri Kombo aliipongeza Denmark kwa kuwa mshirika wa muda mrefu na wa kuaminika wa Tanzania, akieleza kuwa ilikuwa nchi ya kwanza kuanzisha rasmi ushirikiano wa maendeleo na taifa hili. Aidha, alitambua mchango mkubwa wa Shirika la Maendeleo la Denmark (DANIDA) katika kusaidia vipaumbele vya maendeleo ya taifa hususan katika sekta za elimu, afya, maji, na kilimo.

“Uhusiano wetu sasa umebadilika kutoka kwenye msingi wa misaada ya maendeleo na kuwa ushirikiano wa maslahi ya pamoja unaolenga biashara, uwekezaji na maendeleo ya watu,” alisema Kombo.

Kupitia mkakati wake mpya kwa Afrika uitwao Karne ya Afrika, Denmark inalenga kushirikiana kwa usawa na mataifa ya Afrika katika kukuza uchumi wa kijani, kuongeza biashara na kuvutia uwekezaji. Mkakati huo pia unaweka msisitizo kwa mahusiano ya moja kwa moja kati ya watu wa pande zote mbili.

Siku ya Katiba nchini Denmark huadhimishwa kila mwaka tarehe 5 Juni, ikiwa ni kumbukumbu ya siku ambayo Katiba ya mwaka 1849 ilisainiwa na hivyo kumaliza enzi ya utawala wa kifalme wa mabavu. Katiba hiyo ndiyo msingi wa demokrasia ya Denmark hadi leo, ikilinda haki za raia na usawa katika kushiriki mchakato wa kisiasa.

Wadau waliohudhuria hafla hiyo walitumia nafasi hiyo kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Denmark, wakisema ni mfano bora wa mahusiano yanayojengwa kwa misingi ya heshima, uaminifu na maendeleo ya pamoja.



Chapisha Maoni

0 Maoni