Katika kuhakikisha
linaendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani, Shirika la Nyumba la
Taifa (NHC) limefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha mifumo ya
kidijitali inayoboresha huduma kwa wateja wake na kuongeza ufanisi wa ndani ya
shirika.
Akizungumza kuhusu
mafanikio hayo mapema wiki hii, Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Bw. Hamad Abdallah
Hamad, amesema kuwa tangu mwanzo wa mwaka 2021, Shirika lilianzisha
utengenezaji wa mfumo wa kisasa unaojulikana kama “NHC Integrated System – NHC
IS”, uliobuniwa na kutengenezwa na wataalamu wa Kitanzania kwa usimamizi wa
karibu wa Kitengo cha TEHAMA cha Shirika.
“Mfumo huu ni wa
kidijitali, jumuishi na unaziunganisha shughuli muhimu ndani ya Shirika kwa
ufanisi mkubwa. Mpaka sasa mfumo huu umeunganishwa moja kwa moja na mfumo wa
malipo ya Serikali – GePG pamoja na mfumo wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
kwa ajili ya usimamizi wa taarifa za Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT),”
alisema Bw. Hamad.
Ameeleza kwamba mfumo
huo unamuwezesha kujua kila kinachoendelea ndani ya NHC hata akiwa nyumbani
kwake, lengo sasa ni kuuboresha zaidi kwa kutumia akili unde (AI) ili uweze kuwa
na uwezo wa kutoa ripoti.
Pia, Bw. Hamad amesema
kwa sasa mipango inaendelea ili kuunganisha mfumo NHC Integrated System – NHC
IS na mifumo mingine ya Serikali na
taasisi mbalimbali kwa lengo la kurahisisha utoaji huduma na ufanisi wa
kiutendaji kwa ujumla.
Aidha, Shirika hilo
lipo katika hatua za mwisho kukamilisha “NHC Mobile App”, programu ya simu
janja itakayowezesha wateja kuwasilisha maoni na kupata huduma mbalimbali kwa
urahisi. Programu hiyo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi mwezi Julai 2025.
“App hii ya NHC
Mobile App ni muhimu sana maana tunataka kumuwezesha mteja wetu popote pale
alipo duniani kuweza kuangalia nyumba zetu tunazouza na kukodisha na kufanya
maamuzi baada ya kujiridhisha,” alisema Bw. Hamad.
Aidha, NHC imechukua
hatua kadhaa za kiteknolojia kuhakikisha usimamizi thabiti wa rasilimali na
kupunguza udanyanyifu na kudhibiti wizi. Hatua hizi ni pamoja na usimikaji wa
kamera za ulinzi (CCTV) kwenye miradi yote mikubwa pamoja na matumizi ya vifaa
vya bayometriki kudhibiti malipo ya wafanyakazi kwenye miradi hiyo.
“Teknolojia hizi
zimeleta mabadiliko chanya. Tumepunguza gharama za uendeshaji na kuongeza
mapato ya Shirika kupitia usimamizi mzuri wa miradi ya ujenzi na udhibiti wa
matumizi,” alisema Bw. Hamad.
Kwa ujumla, juhudi
hizi zinathibitisha dhamira ya Shirika la Nyumba la Taifa kuendelea kuwa
taasisi ya mfano katika matumizi ya teknolojia ya kisasa kwa lengo la kutoa
huduma bora kwa Watanzania.
0 Maoni