Marufuku ya kutembea na mbwa mitaani yaongezeka Iran

 

Serikali ya Iran imeongeza marufuku ya kutembea na mbwa katika miji kadhaa nchini humo, ikitaja sababu za usalama wa umma pamoja na afya ya wananchi. Hatua hiyo imeibua hisia mseto, hasa miongoni mwa vijana wa mijini wanaoendelea kumiliki mbwa licha ya vizingiti vinavyowekwa.

Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, marufuku hiyo sasa inatekelezwa katika angalau miji 18, zikiwemo Isfahan na Kerman. Marufuku hii ni mwendelezo wa agizo la polisi la mwaka 2019 lililoweka katazo rasmi la kutembea na mbwa katika mji mkuu wa Tehran.

Mbali na kutembea na mbwa, kusafirisha wanyama hao kwa kutumia magari pia kumepigwa marufuku. Hii ni kwa mujibu wa mamlaka zinazohusika na utekelezaji wa sheria, ambazo zinasema hatua hiyo inalenga kulinda afya na usalama wa raia.

Tangu Mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979, umiliki wa mbwa nchini Iran umekuwa ukitazamwa kwa mtazamo hasi na mamlaka, ambazo zinawaona mbwa kuwa "wachafu" na ishara ya ushawishi wa utamaduni wa Kimagharibi.

Hata hivyo, hali hiyo haijazuia ongezeko la umiliki wa mbwa, hasa miongoni mwa vijana wanaoona wanyama hao kama marafiki wa karibu na njia ya kuonesha upinzani dhidi ya kanuni za utawala mkali wa Kiislamu.

Ingawa hakuna sheria ya kitaifa inayokataza moja kwa moja umiliki wa mbwa, baadhi ya waendesha mashtaka nchini humo wamekuwa wakitoa maagizo ya mitaa yanayotekelezwa kikamilifu na vyombo vya dola.

Kwa sasa, hali hiyo imezua mjadala mkubwa mitandaoni huku wananchi wakitafakari uhuru wao katika maisha ya kila siku ukizidi kudhibitiwa na sera za kihafidhina.




Chapisha Maoni

0 Maoni