MAIPAC yagawa bure Majiko ya gesi Monduli, Lowassa apongeza

 

Taasisi ya Wanahabari ya kusaidia jamii za Asili (MAIPAC) imezindua mpango wa ugawaji bure majiko ya gesi kwa jamii za Asili ili ziweze kutumia nishati safi na salama ya Kupikia na kupunguza matumizi ya kuni.

Mpango huo uliozunduliwa kijiji cha Mbuyuni kata ya Makuyuni wilayani Monduli jana  unalenga kugawa Majiko 1000 ikiwa ni jitihada za shirika hili kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama lakini pia kuunga mkono kampeni ya  Rais Samia Suluhu kuhamasisha matumizi ya nishati safi na Salama nchini. 

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Tasisi ya Smile Youth and Women Support Organization (SYWSO) na kugawa majiko hayo, kijiji cha Mbuyuni wilayani Monduli, Mbunge wa Monduli Fred Lowassa alipongeza MAIPAC na SYWSO kwa kuamua kusaidia jamii.     

 Katika hafla hiyo iliyohudhuriwa na mamia ya watu licha ya MAIPAC kutoa majiko, SYWSO  na MATT Fondation walikabidhi baiskeli za wenye ulemavu, fimbo za kutembelea na vifaa vya shule.

Lowassa alisema moyo wa kusaidia jamii ambao umeoneshwa na mashirika hayo unafaa kuigwa na wakazi wa Monduli na Watanzania kwa ujumla kwani pia aliyekuwa Mkurugenzi wa IPP Hayati Reginald Mengi alikuwa akifanya hjvyo.

Alisema amepata faraja sana kuona wanahabari wameanzisha taasisi za kusaidia jamii na kuanza na wilaya ya Monduli. 

"Mimi binafsi leo nimepata faraja sana kumuona hapa rafiki yangu mwandishi wa habari mahiri   Mussa Juma  kwani siku nyingi tangu nikiwa kijana mdogo nakumbuka kila siku asubuhi tulikuwa tunasubiri kusoma gazeti la _mwananchi_ kujua Mussa Juma ameandika nini,” alisema. 

 Alisema  sasa licha ya kuendelea na kazi ya kutupa habari lakini Juma na wenzake wameamua kuanzisha taasisi za kusaidia jamii nawapongeza sana. 

Alisema wananchi wa Monduli wamepata faraja kupokea misaada hiyo kwani ni mwendelezo wa misaada kwa Jamii.

Alisema Rais Samia Suluhu pia amefanya makubwa katika wilaya hiyo ikiwepo kuleta mradi mkubwa wa maji wa bilioni 27 ambao utasaidia  Kata ya Nanja na vijiji 13 vikiwepo vya kata ya lepurko vya Mbuyuni, Makuyuni na Losimongori.    

Alisema pia kilomita 3 za barabara katika kijiji hicho zimeanza kukarabatiwa na kutatua shida ya barabara.  

 "Lakini pia kutokana na jitihada zangu kama Mbunge niliweza kuonana na Rais Samia kuzungumzia mgogoro wa ardhi ya malisho uliokuwepo hapa Monduli na sasa ametoa uamuzi ardhi hiyo tutatumia kwa pamoja na jeshi letu la wananchi kwa malisho.”    

  "Nawaomba Monduli mwezi Octoba tumpe kura zote Rais Samia kwani ametufanyia mambo makubwa na mengi ikiwepo kutoa fedha sekta za afya, elimu na kusaidia wafugaji," alisema. 

Juma alimshukuru Lowassa kuhudhuria hafla hiyo na kugawa misaada hiyo ambayo inatokana na michango ya taasisi na makampuni ya ndani nchini.

"Mheshimiwa Mbunge misaada hii inatokana ma michango ya Taasisi za kitanzania na ambazo zimeona umuhimu wa kusaidia jamii badala ya kutegemea mashirika kutoka nje ya nchi na sisi MAIPAC tunaomba wadau waendelee kujitokeza kuchangia majiko ili  yasambazwe kwenye jamii hizi za asili,” alisema.

Alisema  Taasisi ya MAIPAC  imekuwa na miradi kadhaa wilaya za Longido, Karatu na Monduli ikiwepo Mradi wa  ujenzi wa uzio chanzo cha maji cha Kabambe kijiji cha Selela ambao umekamilika.   Alisema mradi huo ni sehemu ya mradi wa kulinda, kuheshimu  na kuhifadhi maarifa ya asili ambao unafadhiliwa na Mfuko wa Mazingira Duniani(GEF) kupitia programu za miradi midogo inayoratibiwa na shirika la maendeleo la umoja wa mataifa (UNDP) Tanzania na ofisi ya makamu wa Rais (Mazingira).    

Alisema katika mradi huo MAIPAC hivi karibuni itazindua kitabu cha pili cha maarifa ya asili ya jamii za Asili  za Wadzabe, Datoga na Maasai katika uhifadhi wa Mazingira, Vyanzo vya Maji na Misitu.

Afisa Maendeleo wa halmashauri ya Wilaya ya Monduli, Fauzia Omar alipongeza shirika la MAIPAC na SYWSO kwa kutoa misaada mbalimbali kwa wilaya hiyo na kutaka waendelee kusaidia jamii.

Aliomba mashirika hayo kufika vijiji vyote 62 katika wilaya hiyo, kushirikiana na serikali kusaidia miradi ya jamii lakini pia kutoa elimu ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Chapisha Maoni

0 Maoni