Kutokukamilika kwa ushahidi kwahairisha tena kesi ya Lissu

 

Kesi ya kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Mhe. Tundu Lissu imesikilizwa leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu Jijini Dar es Salaam, huku ikirusha live mtandaoni kesi hiyo kwa mara ya kwanza ili kutoa fursa wa watu wengi zaidi kuifuatilia.

Tofauti na ilivyofikiriwa kwamba pengine shauri hilo lingechukua muda mfupi kwakuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina nguvu ya kisheria ya kusikiliza shauri hilo, badala yake imeshuhudiwa mvutano mkali wa kisheria baina ya mawakili wa pande zote mbili.

Upande wa Jamhuri kupitia Mawakili wake ilianza kwa kuieleza Mahakama kuwa upelelezi wa shauri hilo haujakamilika hivyo kuomba Mahakama kuhairisha kesi hadi siku nyingine, pia Jamhuri iliibua  jambo lingine kwamba mtuhumiwa ameidharau Mahakama hiyo kwani wakati anaingia Mahakamani alitoa manenoya 'No Reforms, No Election' jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

Baada ya hoja hizo za Jamhuri, Mawakili wa utetezi wakiongozwa na Mpale Mpoki, Dkt. Rugemeleza Nshala, Peter Kibatala na wengineo walipinga vikali na kuiomba Mahakama kufuta shauri hilo kwakuwa Jamhuri imeshindwa kukamilisha upelelezi kwa wakati, na kwamba kitendo cha kuchelewesha upelelezi ni kumnyima mteja wao haki zake za msingi ikizingatiwa kuwa kupitia shauri hilo mtuhumiwa hawezi kujibu chochote.

Kuhusu suala la mtuhumiwa kutoa maneno wakati anaingia Mahakamani, Mawakili wake wameileza Mahakama kuwa mtuhumiwa alicheleweshwa kuingizwa kwenye chumba cha Mahakama kwani ameingizwa kwenye chumba hicho sambamba na wakati Hakimu wa kesi husika anaingia, jambo ambalo limemkosesha mtuhumiwa uhuru wa kusalimiana na ndugu, jamaa na marafiki zake waliofika kumuunga mkono

Akitoa maamuzi, baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili, Hakimu anayesikiliza shauri hilo amesema kwa mujibu wa sheria Mahakama inaanza tu pale Hakimu anapokuwa ameingia kwenye chumba cha Mahakama na kwamba kiutaratibu mtuhumiwa anapaswa kuingizwa kwenye chumba cha Mahakama baada ya Mahakama kuanza na si vinginevyo, hivyo kutoa maelekezo kuwa utaratibu huo ndio unaopaswa kufuatwa hata itakapotajwa kwa wakati mwingine.

Kuhusu suala la kutamka maneno wakati Mahakama imeanza, Hakimu amekubaliana na hoja za Jamhuri kuwa ni kweli mtuhumiwa Tundu Lissu ameidharau Mahakama kwa kitendo chake hicho cha kutamka No Reforms, No Election.

Awali Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Tundu Lissu aliingia mahakamani na kauli mbili ya No Reforms, No Election ndani ya chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Jumatatu Juni 2, 2025.

Mahakama imeihairisha kesi hiyo hadi Juni 16, 2025, mtuhumiwa amerejeshwa rumande.

Chapisha Maoni

0 Maoni