Eric Shigongo abuni Madarasa ya Kidijitali, Mapinduzi ya Elimu yaanza Buchosa

 

Kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, wanafunzi wa vijijini sasa wanasoma mubashara na walimu walioko jijini Dar es Salaam kupitia ubunifu wa kiteknolojia ujulikanao kama Darasa Janja.

Mradi huo ambao umebuniwa na Mbunge wa Buchosa, Mheshimiwa Eric Shigongo, unalenga kutatua changamoto ya muda mrefu ya uhaba wa walimu wa masomo ya Sayansi katika shule za pembezoni hasa vijijini kwa kutumia teknolojia kama daraja la elimu.

Kwa kutumia vifaa vya kisasa kama kamera za video, projecta, kompyuta na mifumo ya mawasiliano ya intaneti, wanafunzi kutoka shule mbili tofauti sasa wanaunganishwa moja kwa moja na mwalimu aliyepo jijini Dar es Salaam, wakifundishwa kwa wakati mmoja kana kwamba wote wako katika darasa moja.

“Tuliamua kutotegemea tena ahadi au wahisani. Maendeleo hayawezi kusubiri. Kama Mbunge, niliona kuna njia ya kufanya jambo moja lifanyike sasa – kwa vitendo,” alisema Shigongo katika mahojiano maalum.

Wanafunzi waliopata fursa ya kushiriki katika Darasa Janja wameshuhudiwa wakiongeza ari ya kujifunza, huku baadhi yao wakisema masomo ya Sayansi hayawatishi tena kama zamani.

“Kwa mara ya kwanza tunaona Sayansi ni kitu kinachowezekana. Tunaelewa zaidi kwa sababu tunamuona mwalimu akielezea kwa vitendo,” alisema mwanafunzi mmoja wa Shule ya Sekondari Nyehunge.

Walimu katika shule husika pia wameeleza kufurahishwa na mpango huo, wakisema umewapa nguvu mpya ya kushirikiana kwa karibu na wenzao walioko mjini huku wakijifunza mbinu mpya za ufundishaji.

Mradi huu wa Darasa Janja umetajwa na baadhi ya wadau wa elimu kama mfano wa namna ambavyo teknolojia inaweza kutumika kufungua fursa kwa watoto wa Kitanzania bila kujali walipo.

Katika jamii za vijijini, mradi huu umeleta matumaini mapya. Wazazi, walimu na wanafunzi wameshuhudia jinsi maono ya mtu mmoja, moyo wa kizalendo na uamuzi wa kufanya jambo sahihi yanavyoweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Chapisha Maoni

0 Maoni