Dkt. Mpango atoa wito wa kuchukua hatua za pamoja kulinda bahari

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango, amezitaka nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kushirikiana kwa dhati katika kuchukua hatua za pamoja ili kuendeleza uchumi wa bahari, kupunguza uchafuzi wa mazingira na kulinda bioanuwai ya baharini.

Dkt. Mpango ametoa wito huo leo wakati akihutubia Mkutano wa Tatu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Bahari (UNOC3), unaoendelea katika Jiji la Nice, nchini Ufaransa, ambapo alimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Katika hotuba yake, Makamu wa Rais amesema kuwa ni muhimu kwa mataifa yote kushikamana kimataifa na kuwekeza kwa namna endelevu ili kuimarisha ulinzi wa bahari na kuhakikisha kuwa rasilimali zake zinatumika kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

“Tunapaswa kuchukua hatua madhubuti, sio tu kwa ajili ya mazingira bali pia kwa ajili ya ustawi wa kiuchumi wa mataifa yetu. Bahari ni chanzo muhimu cha maisha, ajira na chakula kwa mamilioni ya watu duniani,” alisema Dkt. Mpango.

Akieleza juhudi za Tanzania katika kulinda mazingira ya baharini, Dkt. Mpango alibainisha kuwa nchi hiyo imeongeza maeneo ya hifadhi ya bahari kwa lengo la kufikia asilimia 20 ya eneo la maji ifikapo mwaka 2030.

Aidha, alieleza kuwa Tanzania inaendelea na utekelezaji wa mikakati ya uhifadhi na usimamizi shirikishi unaoongozwa na jamii, kwa kushirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wananchi wa maeneo ya pwani. “Ushirikiano huu umeongeza hamasa ya jamii kuilinda na kuithamini bahari, kwa kuwa wanajiona kuwa ni sehemu ya suluhisho,” aliongeza.

Mkutano huo wa UNOC3 unalenga kuunganisha juhudi za kimataifa katika kukabiliana na changamoto zinazoikabili bahari ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira na uvuvi haramu.

Tanzania ni miongoni mwa mataifa yanayopakana na Bahari ya Hindi, ikiwa na fursa na changamoto nyingi zinazohusiana na matumizi ya rasilimali za baharini, hivyo kushiriki kwake katika mikutano ya namna hii kunalenga kuimarisha ushiriki na ushawishi wa nchi katika ajenda za kimataifa kuhusu bahari.

Chapisha Maoni

0 Maoni