Daraja la “JP Magufuli” kete nyingine ya utalii kanda ya ziwa

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan, Juni, 19 2025 alizindua daraja la “JP Magufuli” ambalo hapo awali lilifahamika kama Kigongo- Busisi lenye urefu wa Kilomita 3 pamoja na barabara unganishi zenye urefu wa km 1.66 huku ikigarimu shillingi Billioni 718.

Uzinduzi wa daraja hili la kimkakati unaendeleza adhma ya Rais Samia katika kuchochea maendeleo ya mikoa ya Kanda ya Ziwa hususani mikoa ya Mwanza,Geita,na Kagera Kiutalii na Kiuchumi.

Akizungumza na wanahabari baada ya uzinduzi wa Daraja hilo Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Musa Nassoro Kuji alisema kuwa kuzinduliwa kwa daraja hilo linakwenda kuboresha mazingira ya biashara hususani biashara ya usafirishaji na utalii wa Kanda ya Ziwa hususani katika Hifadhi za Taifa Kisiwa cha Rubondo, Kisiwa cha Saanane , Hifadhi ya Taifa Burigi - Chato, Rumanyika -Karagwe na Ibanda - Kyerwa.

"Daraja hili la JP Magufuli linaenda kuongeza ufanisi zaidi katika utalii wa Kanda ya Ziwa na maendeleo ya biashara. Awali wageni katika Hifadhi za Kanda ya Ziwa walitumia muda mrefu kusubiri vivuko ili kuyafikia maeneo ya Hifadhi za Taifa  zilizopo katika mikoa ya kanda ya ziwa adha ya kusubiri vivuko kwa lisaa limoja mpaka mawili sasahivi imekwisha.”

“TANAPA tunapenda kumshukuru Rais Samia kwa namna ambavyo anaipambania sekta ya utalii.

Uwepo wa daraja hili ni kete nyingine kwa Utalii wa Nchi yetu hususani Kanda ya Ziwa, tumeshuhudia Royal Tour na Amazing Tanzania na sasa Rais anaboresha miundombinu ya Barabara ambazo ni nyenzo muhimu katika Utalii” alisema Kamishna Kuji.

Serikali ya Awamu ya Sita imeendeleza adhma ya kuboresha miundombinu ya Barabara ambapo imetekeleza ujenzi wa madaraja mengine makubwa (9) ikiwemo daraja la Tanzanite - Dar es Salaam.

                Na. Edmund Salaho - Busisi, Sengerema

Chapisha Maoni

0 Maoni