Midoli ya Labubu yagombaniwa majuu na kuibua hofu

 

Wakati huku Afrika tumezoea kuona watu wakigombania bidhaa mbalimbali muhimu za majumbani wakati kunapotokea uhaba wake, wenzetu majuu hali ipo tofauti, ndio maana kuna baadhi ya watu husema majuu kweli hamnazo. Hivi unaweza kuamini watu wazima wanaweza kugombani midoli ?.

Hali ipo hivi mashabiki wa midoli maarufu ya Labubu wameonyesha hasira zao mitandaoni baada ya mtengenezaji wake kuondoa midoli hiyo kwenye maduka yote nchini Uingereza kufuatia ripoti za wateja kupigania bidhaa hizo, ama kweli ukistaajabu ya Musa utaona ya Firauni.

Kampuni ya Pop Mart, inayotengeneza midoli hiyo ya mnyororo wa begi yenye umbo la monsteri, iliambia BBC kuwa imesitisha uuzaji wake katika maduka yake yote 16 hadi mwezi Juni ili "kuepusha matatizo yoyote ya usalama yanayoweza kutokea".

Shabiki wa Labubu, Victoria Calvert, amesema alishuhudia vurugu katika duka la Stratford mjini London. "Ilikuwa ni hali ya kutisha kuwa katika mazingira ambayo watu walikuwa wanapigana na kupiga kelele – na ilisababisha hofu."

Midoli hiyo laini ilianza kuwa maarufu kwenye TikTok baada ya kuvaliwa na watu mashuhuri kama Rihanna na Dua Lipa. Sasa baadhi ya wataalamu wa rejareja wanatoa tahadhari kuwa kusitishwa kwa bidhaa hizo kutazidisha tu uhitaji.

Mdoli Labubu ni kiumbe wa ajabu aliyechorwa na msanii wa Hong Kong, Kasing Lung, mzaliwa wa Hong Kong, na alijulikana zaidi kupitia ushirikiano na duka la midoli la Pop Mart. Tangu walipopata umaarufu wa watu mashuhuri, midoli hiyo imekuwa maarufu kama vifaa vya mitindo.

Nchini Uingereza, bei zake huanzia £13.50 (Tsh 47,320) hadi £50, (Tsh 182,000) huku matoleo adimu yakiuzwa kwa mamia ya pauni kwenye tovuti za uuzaji tena kama Vinted na eBay.


   Msanii wa Hong Kong, 
Kasing Lung, ambaye ndiye mbunifu aliyechora kiumbe cha ajabu cha midoli ya Labubu 

Chapisha Maoni

0 Maoni