Wizara ya Maliasili na Utalii inatarajia kutangaza baadhi ya
maeneo yaliyotumiwa na wapigania uhuru wa kusini mwa Afrika kuwa vivutio vya
utalii wa kihistoria, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kukuza na kuendeleza sekta
ya utalii nchini.
Naibu Waziri wa
Maliasili na Utalii, Mhe. Dunstan Kitandula ameyasema hayo bungeni leo
alipokuwa akijibu swali la Mhe. Dkt. Rita Kabati, ambaye ametaka kufahamu iwapo
kuna mpango wa kuyatambua na kuyaendeleza maeneo kama Kihesa Mgagao (Kilolo)
ili yawe vivutio vya utalii.
Mhe. Kitandula akijibu swali hilo, amebainisha kuwa maeneo
kama Kihesa Mgagao – Kilolo na Mazimbu – Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine, Kampasi
ya Mazimbu, tayari yamepata ridhaa kutoka kwa wamiliki wake ili yachukuliwe
hatua stahiki na kutangazwa kuwa sehemu ya urithi wa taifa.
Aidha, ameongeza kuwa Wizara inaendelea na zoezi la kubaini
maeneo yenye historia na umuhimu wa kihistoria ambayo yanaweza kuendelezwa kama
vivutio vya utalii. Maeneo hayo yanajumuisha yale yanayomilikiwa na Halmashauri
za Manispaa na Wilaya, Taasisi za Serikali na binafsi, pamoja na jamii na
familia mbalimbali. Baada ya utambuzi huo, Serikali huanzisha majadiliano na
wamiliki ili kuweka mikakati ya kuyaendeleza.
"Tanzania, chini ya uongozi wa Awamu ya Kwanza wa
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ilijipambanua kuwa mstari wa mbele katika
harakati za ukombozi wa nchi nyingi za Kusini mwa Afrika. Serikali ya wakati
huo ilitoa maeneo maalum kwa wapigania uhuru kwa ajili ya kujenga makambi ya
mafunzo ya kiitikadi na kijeshi, ambapo wataalamu kutoka ndani na nje ya nchi
walihusika katika kuwaandaa wapambanaji wa ukombozi wa mataifa
yao,"amesema.
Amesema hatua hiyo ya Serikali inalenga kuhifadhi historia, kuuenzi mchango wa Tanzania katika ukombozi wa Afrika, pamoja na kuvutia watalii wa ndani na nje wanaopenda kujifunza historia ya bara hilo.
Na. Anangisye Mwateba - Dodoma



0 Maoni