Mloganzila yatoa uvimbe kwenye pafu kwa kutumia matundu madogo

 

Kwa mara ya kwanza wataalam wazawa Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila wamefanya upasuaji wa kuondoa uvimbe kwenye pafu la mgonjwa kwa njia ya matundu madogo (Thoracoscopy).

Kwa mujibu wa Mkuu wa Idara ya Upasuaji MNH-Mloganzila Dkt. Eric Muhumba huduma hiyo ya ubingwa bobezi imefanywa na wataalam wa Muhimbili Mloganzila kwa kushirikiana na Muhimbili Upanga ambako huduma hii ilianza kutolewa.

Dkt. Muhumba ameongeza kuwa manufaa ya huduma hiyo ni pamoja na mgonjwa kupunguza  maumivu wakati na baada ya upasuaji, kupunguza muda wa kukaa hospitalini hususani wodi ya uangalizi maalum, mgonjwa kutokuwa na kidonda kikubwa na makovu makubwa.

“Tumekuwa tunatoa huduma hizi hapo awali kwa kufungua kifua na kutoa uvimbe lakini kwa mara ya kwanza tumefanikiwa kutumia matundu madogo na mgonjwa anaendelea vizuri, wataalam tunaendelea kumfuatilia kwa karibu,” amesema Dkt. Muhumba.

Dkt. Muhumba amebainisha kuwa kufanikiwa kwa huduma za ubingwa bobezi zikiwemo za matundu madogo kumetokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa katika sekta ya afya ikiwemo kusomesha wataalam, uwepo wa vifaa tiba vya kisasa vya kutolea huduma na mazingira wezeshi na rafiki ya kufanyia kazi.

Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila imejipambanua kwa kuanzisha huduma nyingi za ubingwa bobezi na kuwapunguzia Watanzania usumbufu na gharama kwenda nje ya nchi kutafuta huduma hizo na kuwavutia watu mbalimbali kutoka mataifa jirani kunufaika na huduma zilizopo nchini.

Chapisha Maoni

0 Maoni