Kiwanda cha mafuta ya parachichi Njombe chawakomboa wakulima

 

Mkuu wa Wilaya ya Wanging'ombe mkoani Njombe, Bw. Zakaria Mwansasu, amesema kwamba kiwanda cha kuchakata mafuta ya parachichi cha Avoafrica kimekua mkumbozi wa wakulima wa parachichi wa mkoa huo na mikoa jirani.

Bw. Mwansasu ameyasema hayo jana wakati wanachama wa Jukwaa la Wahariri Tanzania walipotembelea kiwanda hicho wakiwa nji njiani kurejea Dar es Salaam kutoka Ruvuma, kwa mwaliko wa Mkuu wa Mkoa Njombe Mhe. Anthony Mtaka.

Amesema kwamba zamani wakulima walikuwa wanakosa mahali pa kuuzia parachichi ambazo hazijakidhi vigezo vya kuuzwa nje ya nchi na kujikuta wakipata hasara kutokana na kukosa wateja ama kuuza kwa bei ya chini mno.

Amesema kwamba tangu kuanzishwa kwa kiwanda hicho cha Avoafrica sasa mambo yamebadilika kwani wakulima wamepata soko la uhakika la parachichi ambazo hazikidhi mahitaji ya soko la nje ya nchi na matokeo yake kuchochea kasi ya ukuaji wa kilimo cha zao hilo.

Kwa upande wake Meneja Rasilimali Watu wa Kiwanda hicho Megan Kabuje akiongea kwa niaba ya meneja wa kiwanda hicho amesema kwa sasa wananunua parachichi hizo kwa bei ya shilingi 700 kwa kilo na bei itaendelea kuongezeka kadri ya muda unavyokwenda.

“Hapo awali wakulima wa parachichi walikuwa wakipata hasara kwa kukosa soko na hata waliobahatika kuuza walikuwa wakiuza kwa shilingi 100 kwa kilo, lakini sasa wamepata soko la uhakika kwa kuuza shilingi 700 kwa kilo,” alisema Bw. Kabuje.



Chapisha Maoni

0 Maoni