Hakuna mwenye uwezo wa kuzuia uchaguzi usifanyike- Dkt. Nchimbi

 

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema kwamba hakuna mtu yeyote mwenye mamlaka ya kusema uchaguzi mkuu usifanyike, hivyo uchaguzi mkuu wa mwaka huu utafanyika kama ulivyopangwa.

Dkt. Nchimbi ametoa kauli hizo leo mkoani Songea wakati akifungua Mkutano Mkuu Maalum wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), ambapo alikua akigusia kampeni ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ya No Reform No Election inayoendeshwa na Mwenyekiti wake Tundu Lissu.

“Naomba nizungumzie kidogo kuhusu No Reforms, No Election, tumekuwa tukifanya uchaguzi mkuu kila baada ya miaka mitano kwa zaidi ya miaka 60, hivyo katika nchi hii hakuna mtu yeyote, hata rais mwenye mwenye uwezo wa kuzuia uchaguzi mkuu usifanyike,” amesema Dkt. Nchimbi.

Amesema pia ameanza kuona kuna watu wanawalazimisha CHADEMA washiriki uchaguzi mkuu, “Ni kosa kumlazimisha mtu kushiriki uchaguzi mkuu kwa kuwa ni haki yake kuamua kushiriki ama kutoshiriki, ila namuomba ndugu yangu Lissu anapogoma kushiriki asiache haki yake ya kuchagua namuomba kura yake.”

“Kama wanagomea kuchagua kugomea uchaguzi waacheni ni haki yao msiwalazimishe, hata hivyo wakina Lissu wanapaswa kujua kama hawajashiriki uchaguzi wa mwaka huu kuna chaguzi nyingine zitakuja baada ya miaka mitano watakapoamua kushiriki watashiriki,” amesema Dkt. Nchimbi.



Chapisha Maoni

0 Maoni