Balozi Tembele ashiriki Mdahalo wa Miaka 70 ya Mkutano wa Asia na Afrika

 

Mheshimiwa Macocha M. Tembele, Balozi wa Tanzania nchini Indonesia ameshiriki katika Mdahalo maalum kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 70 ya Mkutano wa Afrika na Indonesia maarufu kama Mkutano wa Bandung.

Mdahalo huo uliofanyika jana umeandaliwa na Kituo cha Mikakati na Masomo ya Kimataifa (Center for Strategic and International Studies- CSIS) cha Indonesia na kuongozwa na kaulimbiu isemayo The Global South in a Shifting World Order: Challenges, Aspirations, and the Road Ahead.

Aidha, mdahalo huo umehudhuriwa na Mheshimiwa Arif Havas Oegroseno, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Indonesia pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo mabalozi, wahadhili wa vyuo vikuu, wanafunzi n.k.

Kwa upande wake Mheshimiwa Balozi Tembele pamoja na mambo mengine alibainisha kuwa, Tanzania ni miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa zilizoshiriki kikamilifu katika utekelezaji wa misingi ya ushirikiano, mshikamano, usawa na ukombozi zilizoasisiwa katika Mkutano wa Bandung wa mwaka 1955 kupitia ushiriki wake katika uanzishwaji wa Umoja wa Nchi zisizofungamana na Upande Wowote (NAM), pamoja na harakati za ukombozi wa nchi za Afrika.

Vilevile, Mheshimiwa Balozi alizungumzia kuhusu umuhimu wa mataifa ya Ulimwengu wa Kusini kudumisha fikra za Bandung kwa kuimarisha zaidi ushirikiano kiuchumi kupitia Taasisi na Jumuiya zake za Kikanda kama vile Umoja wa Afrika (AU) na ASEAN. 

Halikadhalika, Mheshimiwa Balozi alitoa wito kwa nchi za Ulimwengu wa Kusini kuangalia uwezekano wa kuzifanyia mapitio agenda za Bandung ili ziweze kuakisi hali ya sasa ya kidunia na kuendana na mabadiliko mbalimbali yanayotokea duniani kwa kujumuisha maeneo mapya ya ushirikiano kama vile mabadiliko ya tabianchi n.k.



Chapisha Maoni

0 Maoni