Shirika la TRC lapata hasara ya Tsh Bilioni 224 - CAG

 

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Dkt. Charles Kichere, amewasilisha ripoti yake ya mwaka wa fedha 2023/2024 kwa Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan Ikulu Jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine amesema Shirika la Reli Tanzania (TRC) lilipata hasara ya shilingi bilioni 224 ikilinganishwa na hasara ya shilingi bilioni 102 mwaka uliopita.

“Shirika la Reli Tanzania (TRC) lilipata hasara ya shilingi bilioni 224 ikilinganishwa na hasara ya shilingi bilioni 102 mwaka uliopita, hasara hii ilichangiwa na kupungua kwa mapato ya usafirishaji kutokana na uhaba wa vichwa vya treni na mabehewa pamoja na mvua kubwa iliyosababisha kufungwa kwa njia kwa miezi minne,” amesema Dkt. Kichere.

Ameongeza kwa kusema kwamba “Shirika lilitumia shilingi bilioni 29.01 ikiwa ni ruzuku kutoka Serikalini, kama ruzuku hii isingetolewa Shirika lingepata hasara jumla ya shilingi bilioni 253.”

Dkt. Kichere amefafanua kwamba taarifa hiyo inahusu kipindi kinachoishia June 30, 2024 kabla ya kuanza kutumika kwa treni za SGR kwa hiyo mapato ya SGR hayapo humo.

Pia Dkt. Kichere akatoa ushauri kwa TRC ijikite katika kuboresha ufanisi wa utendaji kazi wake ili kuongeza ukusanyaji wa mapato na kutekeleza hatua madhubuti za kupunguza gharama, iandae mpango wa kina wa kupata injini za treni na mabehewa ili kukidhi mahitaji ya usafirishaji ipasavyo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2023/24 kutoka Bw. Charles Kichere kwenye hafla fupi iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Machi, 2025.


Chapisha Maoni

0 Maoni