Wizara ya Maliasili na Utalii yapongezwa kuratibu Tamasha la Vita vya Majimaji

 

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mhe. Kanali Ahmed Abbas Ahmed, ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa uratibu mzuri wa Tamasha la Kumbukizi la Vita vya Majimaji, linalofanyika kila mwaka katika mkoa huo kwa lengo la kuwaenzi mashujaa wa vita hivyo. 

Akizungumza jana katika maadhimisho ya Siku ya Wangoni (Ngoni Day) yaliyofanyika Kijiji cha Maposeni, Kanali Ahmed amesema kuwa siku hiyo ni mwendelezo wa matukio kuelekea kilele cha kumbukizi ya mashujaa waliopoteza maisha yao katika harakati za kupinga utawala wa kikoloni wa Kijerumani. 

Amesema uratibu wa tamasha hilo umeendelea kuwa wa kiwango cha juu kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa pamoja na Baraza la Mila na Desturi. Mafanikio haya yanadhihirika kwa mwitikio mkubwa wa wananchi, jambo linaloonesha uzalendo na heshima kwa mashujaa wetu, alisema Kanali Ahmed. 

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kumbukizi hizo kuwa ni  njia ya kuwaenzi mashujaa 67 waliopoteza maisha yao wakipigania uhuru wa Taifa. 

“Leo tupo hapa tukifurahia matunda ya amani, rasilimali, mila na tamaduni zetu. Haya yote ni matokeo ya kujitolea kwa mashujaa wetu, hivyo ni muhimu kuendelea kuwaenzi kwa vitendo,"alisisitiza. 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Malikale na Makumbusho kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. William Mwita alieleza kuwa wizara itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha tamasha la kumbukizi ya mashujaa wa Vita vya Majimaji linaendelea kuimarika na kuwa chachu ya uzalendo kwa Watanzania. 

“Uwepo wa Makumbusho ya Majimaji ni darasa muhimu kwa Taifa letu katika kuhifadhi historia na urithi wa kihistoria. Ni wajibu wetu kulinda rasilimali zetu na kuzihifadhi kwa kizazi cha sasa na kijacho,"alisema Mwita. 

Aidha, alitoa wito kwa wananchi wa Ruvuma kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kilele cha maadhimisho ya kumbukizi hizi, kama walivyoshiriki kwa hamasa kubwa katika mashindano ya ngoma za asili, kongamano la kihistoria, na maadhimisho ya Siku ya Wangoni.

   Na. Said Lufune - Ruvuma


Chapisha Maoni

0 Maoni