Serikali yapongezwa ujenzi wa barabara kiwango cha lami Mbambabay

 

Wananchi wilayani Nyasa mkoani Ruvuma, wameipongeza Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa kuboresha miundombinu na kujenga barabara za mitaa katika mji mdogo wa Mbambabay kwa kiwango cha lami.

Wamesema, ujenzi wa barabara hizo umesaidia kurahisisha huduma ya usafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine, kuondoa adha ya vumbi kipindi cha kiangazi na matope kila inapofika msimu wa mvua pamoja na maeneo yao kupanda thamani ikilinganishwa na siku za nyuma.

Petro Zambala mkazi wa Mbambabay alisema, uamuzi wa Serikali kujenga barabara kwa kiwango cha lami katika mji huo utaharakisha maendeleo na kuchochea kukua kwa uchumi wa mtu mmoja mmoja na wilaya ya Nyasa.

“Ni jambo la faraja kwetu kujengewa barabara za lami kwenye mitaa yetu, kukamilika kwa barabara hii kumesaidia kupunguza gharama za maisha na usafiri.”

Bw. Nikaya Mbalale mkazi wa Mbambabay alisema, tangu Serikali ya awamu ya Sita ilipoingia madarakani kuna mabadiliko makubwa katika mji huo hasa baada ya TARURA kupatiwa fedha nyingi ambazo zimewezesha kuboresha miundombinu ya barabara za lami, tofauti na siku za nyuma ambapo barabara nyingi za mitaa zilikuwa za vumbi.

Alisema, kuimarisha na kuboreshwa kwa barabara hizo zimehamasisha na kuwavutia watu wengi kwenda kuwekeza katika Mji wa Mbambabay ambao wananchi wake wanategemea shughuli za uvuvi na kilimo ili kuendesha maisha yao.

Alisema, Serikali imemaliza kero hiyo, sasa magari yanafika na kuondoka kwenye mji wa Mbambabay muda wowote na wananchi wanafanya shughuli zao za uzalishaji mali.

Kaimu Meneja wa TARURA Wilaya ya Nyasa, Mhandisi Derick Theonest alisema, TARURA inaendelea kufanya jitihada mbalimbali kwa kujenga barabara za lami ili kuboresha mazingira na maisha ya wananchi wa mji wa utalii wa Mbambabay na wilaya ya Nyasa kwa ujumla.

Alisema, hadi sasa wamebakisha kilometa1 ili kukamilisha barabara za lami katika mji wote wa Mbambabay na kuishukuru Serikali kwa kuendelea kuipatia TARURA fedha kwa kujenga miundombinu ikiwemo barabara za lami ambazo zina mchango mkubwa katika kuchochea na kuharakisha maendeleo.

Amewataka wananchi kuhakikisha wanatunza na kulinda miundombinu ya barabara hizo ili ziweze kudumu kwa muda mrefu kwani zinatumia fedha nyingi kuzijenga.

Chapisha Maoni

0 Maoni