Mloganzila kufanya kambi maalum ya upasuaji nyonga na magoti

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila imeandaa kambi maalum ya upasuaji wa marejeo (revision) wa kupandikiza nyonga na magoti kuanzia Februari 26 hadi Machi 07, 2025.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Upasuaji Dkt. Godlove Mfuko kambi hiyo itafanywa na wataalam wa Muhimbili Mloganzila kwa kushirikiana na Daktari Bingwa Mbobezi wa Upandikizaji wa Viungo kutoka nchini China Prof.Tian Hua.

Dkt. Mfuko amebainisha kuwa hospitali imeamua kuanzisha huduma hizo za marejeo kutokana na uhitaji wa watu wengi wanaokuja kutafuta huduma hiyo hospitalini hapo na kutofanikiwa hivyo uongozi ukaona ipo haja ya kuwapunguzia usumbufu wa maumivu na gharama za kutafuta huduma hizi nje ya nchi.

“Serikali imeendelea kuwajengea uwezo wataalam wa ndani ili kufanya huduma za ubingwa bobezi kama hizi, sasa ni wajibu wetu sisi kama wataalam kuanzisha huduma mpya kwa lengo la kuwapunguzia gharama na usumbufu wananchi kwenda kutafuta huduma hizi nje ya nchi. Awali upasuaji huu ulikua haufanyiki hapa nchini kutokana na upatikanaji wa nyonga na magoti bandia maalum kwa ajili ya upasuaji wa marejeo pamoja na utaalam,” ameongeza Dkt. Mfuko.

Dkt. Mfuko amesema kuwa huduma za marejeo za upandikizaji wa nyonga na magoti hufanyika kutokana na nyonga na magoti yaliyowekwa mwanzo kusagika au changamoto zingine na kuongeza kuwa kwa wale wanaohitaji huduma hizi wafike hospitalini mapema kwa uchunguzi na hatimaye matibabu.

Hospitali ya Taifa Muhimbili imefanya huduma za upandikizaji wa nyonga na magoti kwa zaidi ya wagonjwa 256 tangu huduma hizo zilipoanza kutolewa hospitalini hapa mwaka 2023.

Chapisha Maoni

0 Maoni