Wadau wa kuongoa shoroba wajifungia Arusha

 

Serikali imezitaka Taasisi na wadau wa sekta ya Utalii kushirikiana kwa pamoja katika kukwamua rasilimali za wanyamapori kupitia shoroba mbalimbali nchini kwa manufaa ya jamii na Taifa kwa ujumla.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dunstan Kitandula (Mb) wakati akifungua mkutano wa pili wa siku tatu wa jukwaa la wadau wa kuongoa shoroba unaofanyika jijini Arusha.

Mhe. Kitandula amesema jitihada zinazofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau wa uhifadhi zinaweza zisizae matunda ikiwa  jamii  zinazoishi karibu na hizo shoroba hazitashirikishwa kwenye uhifadhi kwani maarifa pamoja na uwakilishi wao wa kuishi maeneo hayo ni kielelezo na kiungo muhimu cha uhifadhi endelevu.

Mhe. Kitandula ameongeza kuwa wizara inaendelea kufanya juhudi kubwa ikiwemo kutengeneza mkakati wa kufanya tathmini, kuweka viupaumbele pamoja na mpango kazi wa miaka mitano (2022-2026) ambapo Shoroba 61 zimetambuliwa na 20 zimewekewa mkakati wa  kipaumbele kwa kuwa ziko hatarini kutoweka licha ya kuwa na umuhimu mkubwa wa kiikolojia na uhifadhi endelevu.

“Ni hakika Mjadala utatupa maarifa mapya, uzoefu mpya wenye kuleta suluhisho thabiti lenye kuleta ustawi na utangamano kati ya  jamii zinazoishi karibu na shoroba pamoja na wanyama wanaotumia shoroba hizo kama mapito,” amesema Mhe. Kitandula.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo  Kamishna wa Polisi Benedict Wakulyamba amesema kongamono hilo litasaidia kuchukua hatua  stahiki zitakazosaidia kurejesha muunganisho wa wanyamapori na mifumo ya ikolojia ya wanyamapori kwa ustawi wa jamii na Taifa kwa Ujumla.

“Kama wizara tumetengeneza mpango mkakati wa kuongoa shoroba za wanyamapori ikiwemo kuhakikisha muingiliano kati ya maeneo ya shughuli za binaadamu na njia za wanyama linazibitiwa kikamilifu,” amesema CP Wakulyamba.

Katika hatua nyingine CP. Wakulymba amewashukuru wadau wa kongamano hilo kwa kutenga muda wao kujadili changamoto mbalimbali zinazokumba mapitio ya wanyama (shoroba) ili kupata suluhisho muhimu kwa ajili ya ustawi wa uhifadhi endelevu.

Awali, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Wanyamapori wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Fortunata Msoffe amesema kuongolewa kwa shoroba za wanyamapori itasaidia katika kuongezeka kwa vivutio vya utalii vitakayosaidia ukuaji wa uchumi kupitia utalii na ongezeko la ajira kwa vijana ili kutimiza azma ya serikali ya awamu ya sita chini ya rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutatua changamoto ya ajira kwa vijana.

Kwa upande wake Kaimu mwenyekiti wa kamati ya Kitaifa ya kuongoa shoroba za Wanyamapori ambaye pia ni Mkurugenzi Msaidizi ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Ally Mfikirwa amesema kukutana kwa wadau kupitia kongamano hilo kutaleta manufaa makubwa ikiwemo kutafuta majibu ya kuondoa migongano kati ya binadamu na wanyamapori lakini pia kuokoa maisha ya wanyamapori dhidi ya wananchi katika hifadhi zao.


Chapisha Maoni

0 Maoni