Polisi Kinondoni yawafariji wagonjwa Muhimbili Mloganzila

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni limetembelea na kukabidhi zawadi kwa uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili- Mloganzila kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa wasio na uwezo waliolazwa hospitalini hapo.

Akikabidhi msaada huo kwa niaba ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Mkuu wa Polisi Jamii mkoa huo, ACP-Ally Wendo amesema jeshi hilo limeona litoe msaada kwa wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo kwa kutambua kuwa wapo wagonjwa ambao  hawana uwezo kabisa.

“Zawadi hizi zimetoka kwa Polisi Mkoa wa Kinondoni, tumeona tutoe kile kidogo tulichonacho kwa ajili ya kuwasaidia ndugu zetu wanaopata matibabu hapa, nimeambatana na OCD Kimara pamoja na OCS Kimara (Gogoni), tunaamini zawadi hizi zitaongeza matumaini kwao,” ameongeza ACP Wendo.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi wilaya ya Kinondoni (OCD) SSP-Deogratias Massawe amesema pamoja na kukabidhi msaada huo wamepata fursa ya kupata elimu ya namna ya kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza ambayo yamekuwa tishio kwa siku za karibuni.

Naye, Mkuu wa Idara ya Ustawi wa Jamii Bw. Emmanuel Mwasota amelishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni kwa msaada huo na kuongeza kuwa hospitali hiyo inapokea wagonjwa kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, ambapo wengine ni wale wanaopata ajali barabarani ambao wengi wao ndugu zao hawajulikani na hufikishwa hospitalini wakiwa hawana kumbukumbu sawasawa.

Pamoja na maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Tanzania Bara, Jeshi hilo limetoa msaada huo ikiwa ni kilele cha Siku 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia.

Chapisha Maoni

0 Maoni