Kampeni ya “Twenzetu Kileleni 2024” yavunja rekodi

 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Utalii Nkoba Mabula amesema zaidi ya asilimia 90 ya Wapanda Mlima zaidi ya 250 waliojitokeza kupanda Mlima Kilimanjaro ili kuadhimisha miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania Bara wamefika katika kilele hicho usiku wa kuamkia Desemba 09, 2024.

Ndg. Nkoba ameyasema hayo jana Desemba 10, 2024 katika lango la Marangu lililopo mkoani Kilimanjaro wakati wa hafla ya kuwapokea wapandaji hao walioianza safari ya kukwea jabali hilo tarehe 03 hadi 05/12/2024 wakipitia njia tofauti za Lemosho, Machame na Marangu.

Rekodi hiyo imevunjwa kutokana na wingi wa wapandaji hao kufika katika kilele cha Paa hilo la Afrika lenye urefu wa mita 5,895 kutoka usawa bahari. Mlima Kilimanjaro ni miongoni mwa milima iliyotokana na mlipuko wa Volcano, ukivuta watalii wengi kutokana na upekee wake wa kuwa na barafu kileleni tofauti na milima mingine iliyoko ukanda wa kitropiki.

Akiwa katika hafla hiyo, Naibu Nkoba alisema, “Licha ya wapandaji wengi kufika kileleni, pia kampeni hiyo imehusisha wapanda mlima kutoka mataifa mengine ya Marekani, Austria na China huku ikijumuisha kundi la watu wenye uhitaji maalumu tofauti na miaka ya nyuma.”

Hata hivyo, kampeni hiyo ilijumuisha kundi la wazawa waliopanda kwa kukimbia kwa kutumia masaa 13:02, wengine kutembea kwa kasi na kutumia siku moja tofauti na wapanda mlima wengi waliotumia siku 8 Lemosho, siku 7 Machame na siku 6 Marangu.

Naye, Balozi Dkt. Mahadhi Maalim anayeiwakilisha Tanzania nchini Malayasia na kiongozi wa jopo la mabalozi waliopanda alisema ujio wao utaongeza weledi wa kuujua zaidi mlima huo na kunadi vivutio zaidi ya kivutio cha kupanda mlima huo ikiwemo utalii wa Parachuti, kupanda kwa baiskeli na zao la kupanda kwa kukimbia kama walivyoshuhudia kipindi hiki.

Aidha , Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania(TANAPA) Jenerali (Mstaafu) George Waitara aliwapongeza “Guide”, Wapishi na Wapagazi alimaarufu Wagumu kwa jitihada na uzalendo waliouonyesha kufanikisha zoezi zima la kupanda mlima huo.

“Juhudi zenu na Uzalendo umekuwa nguzo ya kufanikisha zoezi la kupanda mlima huu. Hata hivyo nyinyi ndio chachu ya kukuza utalii huu wa kupanda Mlima Kilimanjaro na sekta nzima ya utalii hususani kwa kanda hii ya Kaskazini,” alisema Jenerali (Mst.) Waitara.

Kwa upande wake, Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara TANAPA Massana Mwishawa aliwasihi watanzania kuendelea kutunza Mlima Kilimanjaro kwa kutokata miti ili kupunguza kasi ya kuyeyuka barafu unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira unaofanywa na binadamu.

"Mlima Kilimanjaro ni tunu ya Taifa na ni chanzo ajira kwa wananchi wanaoishi katika ya Kaskazini, hivyo kuharibika kwa mazingira yake, hakutoathiri Tanzania tu bali pia nchi za Kenya, Uganda, Rwanda na Afrika Kusini ambao hutegemea kuleta wageni na kujipatia kipato”, aliongeza Kamishna Mwishawa.

Hafla hiyo adhimu ya kuwapokea wapanda mlima Kilimanjaro kwa ajili ya kumbukumbu ya Maadhimisho ya miaka 63 ya uhuru wa Tanganyika kupitia kampeni ya “TWENZETU KILELENI” imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, ikiweno Naibu katibu Mkuu  Wizara ya Maliasili na Utalii, Mabalozi kutoka nchi mbalimbali,Jeshi la Wananchi (JWTZ), Bodi ya Wadhamini TANAPA, Viongozi waandamizi wa vyama vya Siasa, taasisi mbalimbali na viongozi wa dini.


 

    Na. Happiness Sam/Kilimanjaro

Chapisha Maoni

0 Maoni