Jela miaka 30 kwa kubaka mwanafunzi

 

Mkazi wa Nkalalo wilayani Kwimba mkoani Mwanza, Nicholaus James (21) amehukumiwa kifungo cha miaka 30 gerazani baada ya kukutwa na hatia ya kumbaka mwanafunzi wa kidato cha nne (jina linahifadhiwa) wa Sekondari ya Taro wilayani humo.

Katika kesi hiyo ya Jinai namba 22882/2024, James ametiwa hatiani na Mahakama ya wilaya Kwimba kwa kosa la kumbaka binti ambaye utambulisho wake unahifadhiwa kwa sababu za kisheria (19) mwanafunzi wa kidato cha 4 shule ya sekondari Taro.

Hukumu hiyo ilisomwa jana tarehe 16/12/2024 na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Kwimba, John Jagadi mbele ya mwendesha mashtaka wa Serikali Juma Kiparo.

Awali, Mwendesha Mashtaka Juma Kiparo aliieleza Mahakama kwamba mshtakiwa alitenda kosa hilo tarehe 07.08.2024, katika Kijiji cha Nkalalo, wilaya ya Kwimba kinyume na vifungu vya 130(1)(2)(a) pamoja na kifungu cha 131(1) cha Kanuni ya Adhabu sura ya 16 ya sheria marejeo ya mwaka 2022.

Mshtakiwa alifikishwa Mahakamani kwa mara ya kwanza tarehe 14.08.2024 na kusomewa shtaka hilo ambalo alilikana na kesi hiyo kuahirishwa hadi tarehe 21.08.2024 kwa ajili ya kusomwa hoja za awali.

Baada ya Mahakama kusikiliza mashahidi watano (5) wa Jamhuri akiwemo Mganga aliyemfanyia uchunguzi binti huyo, Mahakama ilijiridhisha bila ya kuacha shaka kwamba mtuhumiwa alitenda kosa hilo.

Aidha, Mahakama hiyo ilielezwa kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo kwa kumvizia binti huyo wakati amekwenda kuchota maji na kumkamata kwa nguvu kwa kumtishia kummchoma kwa kisu na kisha kumchania nguo zake za ndani.

Baada ya kutiwa hatiani mshtakiwa aliiomba Mahakama imuachilie huru kwa kuwa ni mkosaji wa mara ya kwanza kakini mwendesha mashtaka aliisisitiza Mahakama kumpa adhabu kali mshtakiwa kwa sababu watu wa namna yake ni hatari kwenye jamii na wamekuwa wakididimiza na kukatiza maendeleo ya mabinti wenye ndoto za mafanikio.

Licha ya shufaa hizo za mshtakiwa, Hakimu Jagadi alimuhukumu mshtakiwa kutumikia kifungo cha miaka 30 gerezani.

Chapisha Maoni

0 Maoni