Dkt. Mpango awataka CEOrt kutumia teknolojia zitakazosaidia vijana

 

Makamu wa Rais wa Tanzania Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa wanachama wa CEO Roundtable of Tanzania (CEOrt) kuvumbua njia zinazotekelezeka katika kuhamisha teknolojia zitakazowasaidia vijana ambao ni idadi kubwa ya Watanzania kwa sasa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Mpango amesema hayo jana jioni Novemba 30, 2024 alipomwakilisha Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan katika sherehe ya kufunga mwaka ya CEOrt iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Amesema ni muhimu kuwasaidia vijana katika teknolojia za kijani, kuunga mkono katika tafiti na maendeleo pamoja na kuanzisha vituo atamizi vya teknolojia.

Dkt. Mpango amewasihi kupitia upya vigezo vya kujiunga na CEOrt ili kuongeza idadi ya vijana kutoka biashara zinazochipukia kama vile katika sekta ya Burudani, Tehama na Michezo.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa CEOrt, Santina Benson amesema jukwaa hilo linajivunia hatua mbalimbali za maendeleo ikiwamo kuitisha majukwa ya kujadili maendeleo ya kiuchumi, kupitia sekta za viwanda na biashara.

CEO Roundtable of Tanzania inajumuisha Wakurugenzi na Watendaji Wakuu kutoka Makampuni zaidi ya 200 kutoka sekta mbalimbali nchini ambapo wanachama wake wanachangia katika maeneo ya kukuza na kuendeleza uchumi ikiwemo uchangiaji wa kodi na kuimarisha uongozi nchini kupitia programu za mafunzo.

Chapisha Maoni

0 Maoni