Siku ya Nishati kipindi cha COP 29 yafana huko Baku, Azerbaijan

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati ameongoza kikao cha wadau, na kuhimiza uwekezaji katika nishati safi na mbadala.

Siku ya Nishati ya 15.11. 2024 imefanyika kwa mafanikio makubwa katika Banda la Tanzania mjini Baku, Azerbaijan, ambapo wadau kutoka sekta mbalimbali walikusanyika kujadili masuala muhimu yanayohusiana na nishati na mazingira.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Eng. Felchesmi J. Mramba, alifungua kikao hicho jana Novemba 15, 2024 na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kutatua changamoto za nishati duniani.

Katika kikao hicho, mada mbalimbali zilijadiliwa, na washiriki walielezea umuhimu wa nishati safi na nishati mbadala kama njia bora ya kupunguza uharibifu wa misitu unaosababishwa na utegemezi wa nishati ya mkaa na kuni.

Takwimu zinaonyesha kwamba takribani asilimia 85.7 ya Watanzania wanategemea mkaa na kuni kama vyanzo vya nishati, jambo linaloleta athari kubwa kwa mazingira na misitu ya nchi.

Wadau kutoka taasisi mbalimbali walizungumza kwa pamoja kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika nishati mbadala.Mhifadhi Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Dkt. Elikana John, aliwasilisha mada kwa niaba ya TFS, alisisitiza kwamba suluhu za nishati mbadala kama vile nishati ya jua na upepo zitasaidia kupunguza utegemezi wa mkaa na kunyanyua hali ya maisha ya wananchi.

Aidha, Naibu Kamishna wa Uhifadhi wa TFS, Acc. Zainabu Bungwa aliwakumbusha washiriki umuhimu wa kuwajumuisha vijana katika mikakati ya nishati, akitolea mfano wa "Dar es Salaam Youth Global Climate Change Declaration of 2023", mpango uliowezeshwa kwa ushirikiano kati ya TFS na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Mpango huu umejizatiti katika kuhamasisha vijana kushiriki katika uanzishaji wa miradi ya nishati mbadala na kupigania ulinzi wa mazingira.

Naye Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Eng. Cyprian Luhemeja alifunga kikao hicho kwa kutoa shukrani kwa wadau wote wa ndani na nje ya nchi huku akisisitiza kuwa ushirikiano kati ya sekta za umma, binafsi, na jamii ni muhimu katika kuvutia wawekezaji kwa miradi ya nishati.

Aidha aliwapongeza wadau kwa kujitokeza kwa wingi na kutoa wito kwa sekta mbalimbali kufanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha nishati inafika kwa wananchi wote, ikiwa ni pamoja na maeneo ya vijijini na kwa kila mwananchi mmoja mmoja.

Siku hii ya Nishati ya Dunia imekuwa ni fursa nzuri kwa Tanzania kuonyesha juhudi zake katika kukuza nishati safi na mbadala, na pia inatoa mwito kwa wawekezaji kuwekeza katika miradi ya nishati endelevu, ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi, kijamii, na kimazingira ya nchi.

Chapisha Maoni

0 Maoni