Rais Samia atoa tamko baada ya jengo kuporomoka Kariakoo

Rais Samia Suluhu Hassan amewahakikishia Watanzania kuwa serikali itagharamia matibabu ya majeruhi na kuwasitiri waliofariki katika tukio la kusikitisha la kuporomoka kwa jengo la ghorofa Kariakoo, jijini Dar es Salaam.

Rais Samia amethibitisha kuwa watu 13 wamepoteza maisha katika ajali ya jengo hilo lenye maduka  lililoporomoka jana majira ya asubuhi.

Rais Samia ametumia fursa hiyo kutoa pole kwa ndugu, jamaa, na marafiki wa waathirika wa tukio hilo, na kuwaomba Watanzania wote kuwaweka kwenye maombi wale wote walioathirika na kuwaombea pumziko la amani waliopoteza maisha.

"Mpaka sasa, sababu za kitaalamu za kuporomoka kwa jengo hilo bado hazijachunguzwa na kubainishwa kwani kipaumbele chetu kwanza kilikuwa ni kuwaokoa wenzetu waliokuwamo kwenye jengo hilo," alisema Rais Samia.

Aidha, Rais Dkt. Samia amesema baada ya zoezi la uokoaji kukamilika, anamtaka Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa aongoze timu ya wakaguzi majengo ili wakague eneo lote la Kariakoo na kutoa ripoti kamili ya hali ya majengo katika eneo hilo.

Kwa upande wa Jeshi la Polisi, Rais Samia amelitaka lipate taarifa kamili kwa mmiliki wa jengo lililoporomoka jinsi ya ujenzi ulivyokuwa.

Pamoja na mambo mengine, Rais Samia alisisitiza kuwa serikali imejitolea kuokoa na kuwasaidia waathirika wa tukio hili kwa kila hali, huku akitoa wito kwa wananchi kuendelea kuwa na subira na kuungana katika kipindi hiki kigumu.


Chapisha Maoni

0 Maoni