Makalla aitaka TAMISEMI kutenda haki kwa vyama vyote

 

Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM, CPA Amos Makalla, ameitaka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kutenda haki kwa vyama vyote vilivyosimamisha wagombea katika uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji.

Amesema katika uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika Novemba 27 mwaka huu, wapo wagombea wa CCM ambao wamewekewa pingamizi, hivyo madai ya vyama vya upinzani kwamba wagombea wao pekee ndiyo waliowekewa pingamizi yanalengo la kuwahadaa Watanzania.

Makalla ameyasema hayo leo wakati akizungumza na viongozi na wanachama wa CCM Wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam, ambapo amesisitiza kuwa CCM ipo tayari kushiriki uchaguzi huo na itaibuka mshindi kwani imejiandaa ipasavyo.

“Nitume nafasi hii kuwaomba TAMISEMI ambao ndiyo wasimamizi wa uchaguzi huu, waitendee haki CCM na vyama vingine vyote vitendewe haki. Tunaamini uchaguzi utakuwa huru na haki na atakayeshinda kwa haki, atangazwe.

Amesema kwamba CCM haihitaji upendeleo, haihitaji kubebwa, kwa kuwa ipo tayari kwani walishajipanga kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Taarifa zinasema kuwa jumla ya wagombea Tisa wa Chama Cha Mapinduzi kwenye Halmashauri ya Jiji la Arusha Mkoani Arusha wameenguliwa kwenye mchakato wa Uchaguzi wa serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika Novemba 27, 2024 kutokana na kutokidhi matakwa ya kikanuni na sheria za uchaguzi huo.

Kulingana na Msimamizi wa Uchaguzi, Wagombea hao wamekosa sifa kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mitaa wanayogombea kutokuwepo kwenye orodha ya mitaa inayotambulika na Mamlaka ya serikali za mitaa pamoja na kutoainisha Jinsia zao kwenye fomu walizozijaza.

Miongoni mwa walioenguliwa ni pamoja na Frank Samwel Laizer aliyekuwa anagombea uenyekiti wa Mtaa wa Mbeshere, David Molel aliyekuwa anawania uenyekiti Mtaa wa Olkungu na Mohamed Amir aliyekuwa anawania Uenyekiti wa Mtaa wa Makaburi ya Baniani pamoja na Juma Waziri aliyekuwa mgombea Uenyekiti serikali ya mtaa wa Mkwangwaru B.

Aidha, pia wamo wagombea wa Ujumbe wa serikali za mitaa akiwemo Hayrat Manyanga na Gilbert Massawe ambao pia wameshindwa kuendelea na uchaguzi huo wa baadae mwezi huu kutokana na dosari mbalimbali katika ujazaji wa fomu za kuwania nafasi hizo.

Chapisha Maoni

0 Maoni