Waandishi wa Habari tuungane na Watanzania kujiandikisha- Balile

 

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile ametoa  wito kwa waandishi wa habari nchini kutumia haki yao ya kidemokrasia kujiandikisha na kupiga kura kuchagua viongozi katika ngazi ya serikali za mitaa, vijiji na vitongoji nchini.

Balile ametoa kauli hiyo mara baada ya kujiandikisha kushiriki katika uchaguzi huo wa Serikali za Mtaa. Amejiandikisha Mtaa wa Kitunda jijini Dar es Salaam siku ya Jumamosi, Oktoba 12, 2024.

Mwenyekiti huyo wa Jukwaa la Wahariri amesema waandishi wa habari pamoja na utekelezaji wa majukumu yao wasijisahau kutimiza haki hiyo ya msingi.

“Mara nyingi tumekuwa tukiripoti mambo mengi ya wenzetu, lakini sisi wenyewe tumekuwa tukijisahau. Nitoe wito kwa kila mwandishi wa habari popote alipo kujiandikisha na kujitokeza kupiga kura kuchagua viongozi katika mitaa yetu,” amesema Balile.

Balile pia amevikumbusha vyombo vya habari kufanya ufuatiliaji wa zoezi hilo linavyoendelea pamoja na kutoa elimu ya mara kwa mara kwa wananchi kujitokeza kwa wingi, kwani baadhi wanachanganya utaratibu wa Uchaguzi Mkuu unaosimamiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi  na wa Serikali za Mitaa unaosimamiwa na TAMISEMI, badhi wakidai kadi ya Mpigakura wanayo tayari.

Zoezi la uandikishaji  wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji unaotarajiwa kufanyika Novemba 27, mwaka huu limezinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan siku ya Ijumaa, Oktoba 11, 2024,  jijini Dodoma.

Chapisha Maoni

0 Maoni