TFS yapongezwa na Kamati ya Bunge ya Uwekezaji

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imeipongeza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa mafanikio yake katika kutekeleza majukumu yake.

Pongezi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa kamati, Mhe. Augustine Vumma Hole, wakati wa semina iliyofanyika leo kwa ajili ya kuwasilisha mkakati wa TFS katika kuongeza mapato ya Serikali na kuimarisha uhifadhi.

"Nawapongeza kwa kazi nzuri mnayofanya, ambapo mmekuwa na mchango wa bilioni 25 kwenye mfuko mkuu wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/24," alisema Mhe. Hole.

Meneja Mipango wa TFS, Bi. Neema Mbise, alieleza kwamba mapato ya TFS yameendelea kukua, yakifikia bilioni 165.58 kwa mwaka huu.

Aliongeza kuwa, "uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali na dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndiyo sababu kuu ya ukuaji huu na uhifadhi kuimarika."

Kamishna wa Uhifadhi TFS, Prof. Dos Santos Silayo, alipokea pongezi hizo na kutoa ufafanuzi kuhusu hoja mbalimbali za wajumbe wa kamati.

Prof. Silayo pia alizungumza kuhusu mikakati mbalimbali ya TFS, ikiwemo biashara ya kaboni ambayo inatarajiwa kuleta Dola milioni 65.4 kwa mwaka, kuongeza mapato kupitia utalii wa ikolojia, na kukuza uzalishaji wa mazao ya misitu na nyuki.

"Katika kipindi cha miaka minne, Wakala umeweza kukusanya shilingi bilioni 13.1 kutokana na biashara ya utomvu kutoka mashamba ya miti ya Sao Hill, Buhindi, na Rubya," alisisitiza Prof. Silayo.

Kwa kumalizia, alieleza kuwa TFS itaendelea na usimamizi madhubuti na matumizi endelevu ya rasilimali za misitu na nyuki, kuhakikisha kwamba maendeleo yanafikiwa bila kuathiri mazingira.

Chapisha Maoni

0 Maoni