Tanzania yaridhishwa na ushirikiano wake na Namibia

 

Tanzania itaendelea kuimarisha misingi ya uhusiano wa diplomasia baina yake na nchi ya Namibia katika kuimarisha mahusiano yaliyopo katika nyanja mbalimbali huku mchango wa Tanzania katika uhuru wa Namibia ukitajwa.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Ummy Nderiananga ameyasema hayo jana Oktoba 24 alipotembelea Ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia, ambapo aliambatana na watendaji wa ofisi hiyo kwa lengo la kushiki Mkutano wa Nane wa Ngazi ya Viongozi (High Level Meeting) kuhusu masuala ya kupunguza athari za maafa pamoja na kikao cha tisa cha Jukwaa la Kanda la Afrika la kupunguza athari za maafa.

Naibu Waziri Ummy ameeleza kuwa hatua hiyo imefikiwa kutokana na uongozi makini, na mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyojipambanua kidiplomasia na kuhakikisha mahusiano ya Taifa na nchi nyingine unakuwa wenye manufaa na kuiletea nchi heshima katika nyanja mbalimbali.

“Hakika Tanzania imeendelea kuwa kitovu cha amani na utulivu, hii imetokana na uongozi mahiri wa Mhe. Rais Dkt. Samia kwa miongozo na maelekezo yake katika kuhakikisha nchi inaendelea kujipatia maendeleo,”amesema Mhe. Ummy.

Aidha, katika mazungumzo na mwenyeji wake ambaye ni Afisa Mambo ya Nje Mkuu na Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Namibia Elias Tamba ameeleza kuwa, nchi ya Tanzania itaendelea kushirikiana na Namibia katika masuala mbalimbali kwa kuzingatia urafiki uliopo baina ya Mataifa hayo mawili toka kipindi cha Uhuru wa Namibia ambapo Tanzania inakumbukwa kwa mchango wake.

Ujumbe wa Tanzania nchini Namibia umeongozwa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Ummy Nderiananga akiwa ameambatana na Timu yake kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu akiwemo Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi hiyo Brig. Jenerali Hosea Ndagala, Mkurugenzi wa Tathmini na Ufuatiliaji Ofisi ya Waziri Mkuu Charles Msangi, Msaidizi wa Katibu Mkuu wa ofisi hiyo pamoja na January Kitunsi.



Chapisha Maoni

0 Maoni