Serikali ya Tanzania imeendelea
kuonesha umahiri wake katika masuala ya menejimenti ya maafa nchini kwa
kuzingatia mifumo sahihi ya kukabiliana na maafa na matumizi ya teknolojia ya
kisasa pamoja na miongozo, kanuni na sheria mbalimbali zinazoongoza katika
uratibu wa maafa hayo.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri Ofisi
ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Ummy
Nderiananga wakati akiongea na waandishi wa habari mara baada ya kuhitimishwa
kwa Mkutano wa nane wa ngazi ya viongozi kuhusu masuala ya kupunguza athari za
maafa pamoja na Kikao cha tisa cha jukwaa la kanda la Afrika la kupunguza
athari za maafa na vilivyofanyika jijini Windhoek nchini Namibia.
Naibu waziri Nderiananga ameeleza
kuwa, uwekezaji mkubwa umefanywa na Serikali ya Tanzania hususan katika
kuhakikisha teknolojia inavusha Taifa katika kukabili maafa ambapo Serikali
ilianzisha Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga katika Kituo cha Taifa
cha Operesheni na mawasiliano ya dharura nchini Tanzania ambacho kimeifanya
nchi kuwa mahiri katika masuala ya menejimenti ya maafa hususan katika kuzuia,
kupunguza kujiandaa na kukabili maafa pindi yanapotokea.
Katika hatua nyingine Naibu waziri
Nderiananga amezungumzia kuhusu mkakati wa miaka kumi wa Nishati safi ya
Kupikia ambao utekelezaji wake umeanza mwaka huu hadi 2034, ameeleza kuwa
unalenga kuhifadhi mazingira, kulinda afya kwa kuzuia matumizi ya kuni na mkaa
ili kuepuka athari za mabadiliko ya tabia nchi.
“Suala ya mabadiliko ya tabia nchi
linaathiriwa na ukataji wa miti inayopelekea uharibifu mkubwa wa mazingira na
kuchagiza ukosefu wa mvua za kutosha, uwepo wa ukame unaoathiri uzalishaji wa
chakula, tunampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuzindua
mkakati huo,”alisema.
Amesema moja ya mikakati ambayo
Tanzania imejiwekea ni kuhakikisha zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanatumia
nishati safi ya kupikia ifikapo 2034
"Kama nchi tumejipanga
kuhakikisha Taasisi za Serikali na Mashirika binafsi yanawekeza ipasavyo katika
matumizi ya nishati safi kwa maslahi mapana ya mazingira safi na salama, Afya
zetu na Afrika kwa ujumla, " amesisitiza Mhe. Nderiananga.
Awali akifungua mkutano huo Naibu
Waziri Mkuu na Waziri wa Kazi na Uchukuzi Nchini Namibia John Mutorwa amesema
mikutano hiyo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa ambapo awamu hii imefanyika nchini
Namibia na kuwakutanisha wadau zaidi ya elfu moja wa maafa kwa nchi za Afrika wakiwemo wataalamu
kutoka katika ngazi za kitaifa, Serikali za mitaa, Mashirika ya Umoja wa
Kitaifa na Kimataifa, Asasi za Kiraia, sekta binafsi, taasisi za elimu na
utafiti na wanahabari, na hii imetajwa kuwa ni mafanikio makubwa kwa bara la
Afrika.
“Tunashukuru kwa namna nchi
zilivyojitokeza kushiriki mikutano hii muhimu katika kuhakikisha masuala ya
maafa yanakabiliwa na kuwa na Afrika stahimilivu katika maafa, tunawashukuru
sana Mawaziri mlioweza kushiriki mikutano hii, nasi tumepata heshima kama nchi,
na tunaahidi kuendelea kuimarisha mashirikiano yetu kama Bara la
Afrika,”alisema Mhe. Mutorwa.
Aidha, alitoa rai kwa kila nchi kuona
umuhimu wa kujipanga kukabili maafa bila kujali utofauti na hali za Mataifa ya
Afrika, lengo kuyafikia na kuyaishi malengo na kuwa tayari kusimamia masuala
haya.
0 Maoni