Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Balozi, Dkt. Pindi Chana
(Mb) amesema Wizara imeendelea
kutekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan ya kudhibiti changamoto za Wanyamapori wakali na waharibifu
huku akisisitiza mkakati wa kuongeza
ndege nyuki ili kudhibiti tembo.
Waziri Chana ametoa kauli hiyo leo Oktoba 3,2024 wakati akizungumza na Watumishi wa Hifadhi ya Taifa
Katavi, Wilaya ya Mpanda, Mkoani Katavi.
"Mhe. Rais tayari ametuelekeza kudhibiti wanyama wakali
ikiwemo tembo hivyo tunahamasisha vijana katika vijiji vilivyoko pembezoni mwa
maeneo ya hifadhi kujitokeza kujiandikisha kupata mafunzo ya kudhibiti
Wanyamapori wakali na waharibifu katika Chuo cha Likuyu Sekamaganga kilichopo
Namtumbo Mkoani Ruvuma" amesisitiza Mhe. Chana.
Amesema Wizara ya Maliasili na Utalii inaendelea kujenga
vituo vya askari kuhakikisha kuna uhifadhi endelevu na kudhibiti Wanyamapori
wakali.
Mhe. Chana ameelekeza kwenye vituo vya askari vilivyojengwa
Wilaya ya Kalambo na Mbarali vikamilike kwa wakati na viwe na rasilimaliwatu
ili vifanye kazi iliyokusudiwa.
Aidha, amesema Wizara inaendelea na maboresho mbalimbali ya
kutangaza vivutio vya utalii.
"Tayari tuna maelekezo ya Mheshimiwa Rais kuendelea
kuongeza mapato kutokana na Utalii na tunachangia asilimia 17 ya pato la Taifa
na asilimia 25 ya fedha za nje takribani dola za kimarekani bilioni 3.6," Mhe.
Chana amesema.
Katika hatua nyingine amewapongeza Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya nchi nzima kwa kazi nzuri ya uhifadhi wanayoifanya huku akisisitiza Vijiji kuweka ajenda ya kudhibiti moto, kutunza misitu na mazingira iwe ya kudumu.
0 Maoni