Wizara ya Maliasili na Utalii
imeendelea kutekeleza Maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan yaliyotoka na Maoni ya Tume ya
Haki Jinai ya kuboresha Jeshi la Uhifadhi kwa kutoa Mafunzo ili liweze
kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Misingi ya Sheria na Haki za
Binadamu.
Akitoa mafunzo hayo kwa Askari wa
Jeshi hilo kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Wakala
wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) wa Mikoa
ya Simiyu na Mara, Naibu Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii anayeshughulikia
Maliasili, Kamishna wa Polisi (CP), Benedict Wakulyamba, amewaeleza Askari hao
kwamba Taifa lina imani kubwa nao katika ulinzi na usimamizi wa Maliasili
nchini, hivyo ni vyema wakaitunza tunu hiyo ambayo imetokana na imani ya
wananchi kwao.
Aidha, CP Wakulyamba amewataka Askari
hao kujiepusha na matendo maovu kazini, hususan rushwa na kuwabambikia wananchi
matukio ya uongo, huku akiwashauri kujenga mahusiano mazuri miongoni mwao
pamoja na jamii inayowazunguka yaani ile inayozunguka maeneo ya Hifadhi kwani
wao wanayafahamu maeneo ya Hifadhi kwa asili wati Askari wanayafahamu maeneo
hayo Kitaaluma hivyo ushirikiano huo utarahisisha shughuli za Uhifadhi na
kuleta tija kwa Taifa.
Ameongeza kuwa katika kuimarisha Jeshi
la Uhifadhi hapa nchini, Wizara inaendelea kushirikiana na vyombo vingine vya
usalama, likiwemo Jeshi la Polisi na Jeshi la Wananchi ili kulijengea uwezo wa
kiutendaji.
"Tumeanza kushirikiana na Jeshi
la Polisi katika kuwafundisha askari wetu juu ya kuzingatia kanuni za Haki
Jinai katika kutekeleza majukumu yao. Kanuni hizo ni pamoja na Ukamataji
salama, kuheshumu utu wa binadamu, Sheria za upekuzi na kuhodhi mali za uhalifu
kisheria,” alisema CP. Wakulyamba.
"Ikiwa ni sehemu ya maoni ya Tume
ya Haki Jinai, Jeshi la Uhifadhi litaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi
kwa kuwa linauzoefu katika masuala ya utendaji kazi ikiwemo upelelezi na
kudhibiti ghasia za kijamii (Civil disorder management) kwa mbinu salama zenye
kuzingatia misingi ya Haki zabinaadam, hivyo utaalam wake na uzoefu ni muhimu
kwa ustawi wa sekta ya Maliasili na Utalii," aliongeza CP. Wakulyamba.
Aidha, CP. Wakulyamba amewaagiza
Maafisa wa Jeshi hilo kusimamia vyema nidhamu na uadilifu kwa askari wa Jeshi
hilo, kwani madhara yanayotokana na utendaji mbovu wa baadhi ya askari
hayatakuwa na athari tu kwa maisha yao na familia zao, bali pia yataathiri sifa
njema ya Taasisi na Taifa kwa ujumla.
Katika ziara hiyo, CP Wakulyamba,
licha ya kutoa mafunzo kwa askari hao, ametembelea na kukagua shughuli za
uhifadhi katika Mapori ya Akiba ya Ikorongo/Grumet chini ya TAWA, na Hifadhi ya
Taifa ya Serengeti iliyopo chini ya TANAPA.
0 Maoni