Watanzania watakiwa kutunza mazingira kwa kutumia njia za asili

 

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Bw Patrick Mwalunenge amefungua Tamasha la Utamaduni wa Mtanzania kwa jamii ya Wanyakyusa Kijiji cha Makumbusho jijini Dar es Salaam na kuwaasa Watanzania kutunza mazingira kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Akifungua tamasha hilo jana Bw. Mwalunenge amesema kuwa utunzaji wa mazingira ni wajibu wa kila Mtanzania na kwamba matumizi ya malighafi ya asili yanayopatikana katika maeneo yao yatasaidia kutunza mazingira na kuendeleza utamaduni wa Mtanzania.

"Watanzania ni lazima turudi kwenye matumizi ya vifaa vya asili ili tuweze kutunza mazingira yetu" Amesisitiza Bw. Mwalunenge.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Bi. Frida Kombe amesema malengo ya Tamasha hilo ni kutoa nafasi kwa jamii za Tanzania kuonesha tamaduni zao katika Kijiji cha Makumbusho.

Alisema kwamba “Tamasha la Siku ya Utamaduni wa Mtanzania ni mojawapo ya utekelezaji kwa vitendo wa sheria yetu ya Makumbusho ya Taifa la Tanzania na Malikale lakini pia ilani ya CCM inayoweka bayana ushirikishwaji wa jamii kwenye uhifadhi wa urithi wa Utamaduni na kuutumia urithi huo kama chanzo cha mapato,"

Bi Kombe ameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mhe. Dr. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiongezea Taasisi ya Makumbusho uwezo wa kutekeleza majukumu ya uhifadhi wa urithi wa asili na utamaduni.

Tamasha la Utamaduni wa Mtanzania kwa jamii ya Wanyakyusa litafanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia tarehe 27 hadi 29 Septemba 2024 ambapo wananchi wanaweza kujifunza mila na desturi, vyakula, ngoma na mavazi ya jamii wa Wanyakyusa.Watu wote wanakaribishwa hamna kiingilio.



Chapisha Maoni

0 Maoni