SHIRIKA la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa
kushirikiana na makampuni ya waongoza watalii nchini imepanga kuwapeleka
watanzania zaidi ya 500 katika kilele cha Mlima Kilimanjaro kusherehekea siku
ya uhuru kupitia kampeni ya “Twenzetu Kileleni 2024” ikiwa ni msimu wa Nne wa
Kampeni hiyo ikiwa na Kauli mbiu isemayo “Stawisha Uoto wa Asili Tanzania, Okoa
Barafu ya Mlima Kilimanjaro kampeni ambayo imezunduliwa leo mpaka disemba 4,
2024.
Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara wa
TANAPA, Jully Lyimo amewaeleza wanahabari katika mkutano na vyombo vya Habari
uliofanyika katika ofisi za TANAPA jijini, Dar es Salaam leo kuwa lengo la
kampeni hii ni kusherehekea miaka 63 ya Uhuru, tukio ambalo ni la kihistoria
hufanyika kila mwaka ifikapo Desemba 9.
“Katika sura ya Utalii, TANAPA imekuwa ikitumia fursa hii ya
maadhimisho ya siku ya uhuru kuhamasisha watanzania kupanda mlima Kilimanjaro
na kutangaza vivutio vinavyopatikana katika hifadhi hii kupitia kampeni ya
“Twenzetu kileleni” .Lengo la kampeni hii ni kuhamasisha Watanzania kupanda
mlima ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya uhuru wa Tanganyika.”
“Nichukue nafasi hii kuwahamasisha Watanzania wenzangu
kushiriki upandaji huu ikiwa ni kuonyesha uzalendo na kupenda vivutio vyetu. Kwa
hivyo kwa mwaka huu ni msimu wa nne wa kampeni hiyo, tunatoa hamasa kwa watu
binafsi, watanzania ndani na nje ya nchi, mabalozi, taasisi za Serikali na
binafsi kujitoa kwa ajili ya kuunga mkono juhudi hizi.”
"Kama tulivyofanya mwaka jana jumla ya kampuni tatu
ndio zimejitokeza kushiriki kampeni hii katika msimu huu wa nne Kampuni hizo ni
ZARA Tours, African Zoom na African Scenic," alisema Kamishna Lyimo.
Kampuni ya ZARA TOURS itatumia njia ya Marangu kama
ilivyozoeleka, African Zoom watatumia njia ya Machame na African Scenic
watatumia njia ya Lemosho ambapo idadi ya siku za kupanda mlima huo ni 6 kwa
njia ya Marangu.
Aidha, siku 7 kwa njia ya Machame na kwa Lemosho itakuwa
siku 8 huku Gharama za kupanda mlima zitakuwa ni shillingi 1,55,000/- kwa njia
ya Marangu, shillingi 1,830,000/- kwa njia ya Machame na 2,000,000/- kwa njia
ya Lemosho, aliongeza Kamishna Lyimo.
Afisa Uhifadhi Mkuu Mapinduzi Mdesa kutoka Hifadhi ya Taifa
Kilimanjaro aliwataka watanzania wote kujitokeza katika kuadhimisha sherehe
hizo za uhuru katika kilele kirefu zaidi barani Afrika pamoja na kushiriki
katika juhudi za kuokoa barafu ya Mlima Kilimanjaro.
"Kama mwenyeji wa mlima niwakaribishe watanzania kuja
kushiriki nasi katika sherehe hizi za Uhuru katika Paa la Afrika lakini
tunajukumu la kuokoa barafu ya Mlima Kilimanjaro kwa kustawisha uoto wa asili
kwenye maeneo yetu.”
Aidha, Mdesa aliongeza kuwa tafiti zinaonyesaha kuwa chanzo
cha barafu kuyeyuka Mlima Kilimanjaro ni uwepo wa pepo kavu zinazotokea
baharini na maeneo mengine ya nchi zikifika kwenye ile barafu ya Mlima
Kilimanjaro zinapelekea Barafu ile kupungua ukubwa wake na kutoa rai ya kukijanisha
Tanzania kwa kupanda miti ya asili ili pepo zinazotoka kwenye fukwe ziende na
unyevu na kusaidia barafu iendelee kuwepo.
Historia inaonyesha kuwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania
(JWTZ) limekuwa na utaratibu wa kuadhimisha sherehe za Uhuru wa Tanganyika
tangu ulivyopatikana mwaka 1961. Maadhimisho haya yamekuwa yakifanyika kwa
kupandisha bendera ya nchi yetu katika kille cha Mlima Kilimanjaro.
Tukio hili limekuwa likihusisha kikundi cha wanajeshi wachache wakishirikiana na askari wa Hifadhi za Taifa Tanzania kwa utaratibu wa kampuni ya utalii ya ZARA ambapo kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita maadhimisho haya yalipata sura mpya ya ushiriki wa wananchi na kutambulika kwa jina la "Twenzetu Kileleni" ambapo kwa sasa ni msimu wa nne.
Na.Edmund Salaho- Dar es Salaam
0 Maoni