UNDP yaipongeza Tanzania kwa jitihada za kuhifadhi misitu asilia kupitia mradi wa Bionuwai

Tanzania imepokea pongezi kutoka kwa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa kuboresha uhifadhi wa misitu asilia kupitia Mradi wa Kuimarisha Ustahimilivu wa Bioanuai ya Misitu ya Mazingira Asilia Tanzania Dhidi ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi.

Mwakilishi Mkazi wa UNDP, Shigeki Komatsubara anasema kuwa ziara yao kwenye misitu ya asilia wa mlima wa Hanang' uliokuwa umeathirika na mafuriko yaliotokea Wilaya ya Hanang' mapema mwaka huu, ilithibitisha mabadiliko makubwa na urejeshwaji wa uoto wa asili, ikionyesha jitihada za dhati zinazofanywa na Tanzania katika uhifadhi wa mazingira.

“Katika siku hizi tatu, tumeridhishwa sana na urejeshwaji wa bionuwai katika mlima huu wa Hanang na ujumuishi wa uoto wa asili. Tunaamini tutaendelea kushirikiana katika kuongeza na kukuza fursa za uchumi," anasema.

Serikali ya Tanzania, kupitia Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, imeeleza kuwa itatumia uzoefu uliopatikana kupitia mradi huu kuboresha zaidi uhifadhi wa misitu ya asili, kuongeza thamani ya misitu, na kukuza fursa za uchumi kupitia utalii wa misitu.

Prof. Silayo alisisitiza kuwa, “Misitu hii asilia imekuwa kivutio kikubwa. Kwa mfano, katika msitu wa mlima wa Hanang', wageni wameongezeka, miundombinu imeboreshwa, hewa ni safi, na ulinzi umeimarishwa. Tutahakikisha maeneo haya tunayafungua zaidi kwa ajili ya matumizi bora.”

Aidha, Prof. Silayo aliongeza kuwa, kupitia ushirikiano kati ya TFS na UNDP, Serikali itaweka utaratibu endelevu wa usimamizi wa misitu na kuongeza thamani ya misitu hiyo ya asili huku ikishirikisha wananchi katika juhudi za kuitunza.

Tanzania ina misitu asilia 24, ambapo misitu 19 imeendelezwa kwa ushirikiano wa TFS na UNDP kupitia mradi wa kuimarisha bianowai ya misitu ya mazingira asilia dhidi ya tishio la mabadiliko ya tabia nchi.

Chapisha Maoni

0 Maoni