TANAPA washirikiana na Polisi kufanya usafi Kituo cha Afya Mikumi

 

Katika kuadhimisha miaka 60 ya kuanzishwa kwa Jeshi la Polisi nchini, Kituo cha Polisi Mikumi kwa kushirikiana na maafisa na askari wa Uhifadhi, Hifadhi ya Taifa Mikumi wamefanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kufanya usafi katika kituo cha Afya Mikumi mkoani Morogoro kwa lengo kuyaweka mazingira yawe safi na salama ili kulinda afya ya wagonjwa, wafanyakazi na watumiaji wengine wa eneo hilo.

Zoezi hilo la usafi limefanyika leo Septemba 14, 2024 likiongozwa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi Rehembe SSP Kashorael Mnuo akiwa katika zoezi hilo alisema, “Tumeamua kuungana na Majeshi USU mengine wakiwemo hawa wenzetu maafisa na  askari wa Hifadhi ya Taifa Mikumi ili kuweka mazingira safi na salama kuepuka magonjwa ya milipuko yanayosababishwa na uchafu.”

SSP Mnuo aliongeza kuwa Jeshi la Polisi nchini wamekuwa na desturi ya kushirikiana na vyombo vingine  vya ulinzi na usalama kufanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kufanya usafi katika maeneo haya na mengine mengi kwa lengo la kuwa karibu na jamii katika wiki hii ya kuadhimisha miaka 60 ya kuanzishwa kwa jeshi hilo.

“Tupo kwenye wiki ya maadhimisho ya miaka 60 ya kuanzishwa kwa jeshi letu hapa nchini, tumeamua kushirikiana na wenzetu wa Hifadhi ya Taifa Mikumi kufanya usafi eneo hili la Kituo cha afya ikiwa ni pamoja na kuwapa pole wagonjwa kwani kufanya hivi  ni kuonyesha upendo wetu kwa jamii na pia ni matendo ya huruma ambayo vitabu vyote vya kiimani vinatutaka tufanye,” alisisitiza  Kamanda Mnuo.

Aidha, alisema kuwa kilele cha maadhimisho hayo itakuwa ni Septemba 17  mwaka huu na kwamba mbali na kufanya usafi huo pia watawatembelea watu wenye mahitaji maalumu na kuweza kuwasaidia ambapo aliishukuru Mikumi kwa kuungana nao katika zoezi hilo la usafi.

Naye, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Hifadhi ya Taifa Mikumi, Augustine Massesa alisema kuwa wao kama wahifadhi wanalishukuru jeshi la polisi kwa kuwashirikisha katika zoezi hilo la kijamii ambapo alieleza kuwa Mikumi imekuwa mstari wa mbale katika kushiriki shughuli za kijamii.

Kamishna Massesa alisema kuwa kitendo cha wao kushiriki katika shughuli za kijamii maeneo yanayowazunguka yameendelea kuwa chachu ya kuitangaza Hifadhi ya Taifa Mikumi na kudumisha mahusiano ya kuwafichua baadhi ya wananchi wachache wanaojihusisha na shughuli haramu za ujangili katika Hifadhi hiyo.

“Sisi kama Mikumi tutaendelea kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii kwani kufanya hivi mbali na kuitangaza Hifadhi ya Taifa Mikumi pia ni moja ya njia ya kudumisha mahusiano baina yetu na jamii inayotuzunguka na hivyo kudhibiti ujangili.”

Kwa upande wake Mganga wa kituo hicho cha afya Mikumi Beno Hamfik, kwa niaba ya Mganga Mfawidhi alilishukuru jeshi la polisi pamoja na Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa kuendesha zoezi la usafi ambapo aliomba zoezi hilo la usafi liwe endelevu kila mara hata kwa wadau wengine.

   Na. Zainab Ally - Mikumi

Chapisha Maoni

0 Maoni