TFS yapongezwa kwa upandaji miti shamba la Silayo

 

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imepongezwa kwa kazi kubwa ya upandaji miti inayoendelea katika shamba la miti Silayo. Sambamba na pongezi hizo watumishi wa shamba hilo wamekumbushwa kuwa wana wajibu mkubwa wa kimkakati kupitia upandaji miti ili kuliwezesha taifa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi zinazosababishwa na uharibifu wa mazingira.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dunstan Kitandula alipokuwa akiongea na baadhi ya Viongozi na Askari wa hifadhi ya Misitu wa Geita na Shamba la miti Silayo mkoani Geita ambapo Naibu Waziri yupo mkoani Geita kufanya ziara ya kukagua maeneo ya misitu yaliyoathiriwa na shughuli za kibinadamu.

Vilevile, Mhe.Kitandula alitumia fursa hiyo kuwakumbusha Askari wa Jeshi la Uhifadhi kutimiza majukumbu yao kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za utendaji kazi wao, na kutakiwa kujiepusha na vitendo vya rushwa. "Timizeni majukumu yenu bila kuwaonea watu na muongozwe na hofu ya Mungu; haifurahishi tunaposikia tuhuma mbalimbali zikielekezwa kwa askari wa jeshi letu la uhifadhi wakati wa kutekeleza majukumu yenu" alisisiliza Mhe. Kitandula.

Aidha Mhe. Kitandula alisema Askari wa Jeshi la Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) wanalo jukumu la msingi  la kulinda na kuzuia mashamba na hifadhi za misitu yasivamiwe wala kuharibiwa kwa shughuli za kibinadamu. Hivyo ishini viapo vyenu vya utumishi mkikumbuka kuwa taifa linawategemea.

Vilevile Mhe. Kitandula alisema kuwa watumishi wa wakala wa Huduma za Misitu Tanzania wanatakiwa kubadilika kimtazamo kwa kuacha kufikiria moja ya chanzo kikubwa cha kuingiza mapato kwenye taasisi yao ni kutoa leseni za kuchoma mkaa hivyo amewataka kufikiria ni namna gani mazao ya misitu yanaweza kuchangia zaidi mapato.  Alisema bado ufugaji nyuki na mazao yatokanayo na asali unafursa kubwa ya kuwa chanzo kikubwa cha mapato hivyo iwekwe mikakati madhubuti ya ufugaji nyuki na kuzalisha asali yenye ubora kwa viwango vya kimataifa.

Kuhusu fedha za miradi ya huduma kwa jamii Mhe. Kitandula ameagiza kuwa fedha zote zinazotolewa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania zifuatiliwe kwa karibu na kufanya tathimini ili kujiridhisha kama miradi iliyofadhiliwa ina ubora unaolingana na thamani ya fedha zilizotolewa kutekeleza miradi hiyo.

Awali akimkaribisha katika Mkoa wa Geita Mhe. Martin Shighella alimshukuru Naibu Waziri kufika katika Mkoa anaouongoza ili kujionea changamoto ya uharibifu wa misitu katika hifadhi ya msitu wa Geita.

Mhe. Shighella alisema kuwa changamoto yauharibifu wa misitu katika mkoa wa Geita inachangiwa na shughuli za kibinadamu hasa uchimbaji wa madini unaoendelea katika mkoa huu kwa kuwa ndio shughuli kubwa ya kiuchumi kwa wananchi wa Mkoa wa Geita.

Na. Anangisye Mwateba- Katoro- Geita

Chapisha Maoni

0 Maoni