Serikali
imewapongeza wananchi wa tarafa ya Ngorongoro mkoani Arusha kwa kuendelea
kudumisha umoja, amani na utulivu katika eneo hilo na hivyo kuendeleza falsafa
ya R4 ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu
Hassan ya kutaka wananchi wote kuishi kwa maelewano na maridhiano.
Akizungumza
mara baada ya ibada ya shukrani iliyofanyika katika Kanisa katoliki la
Mtakatifu Luka lililopo katika kata ya Endulen wilayani Ngorongoro mkoani
Arusha mshauri wa Rais wa masuala ya siasa na uhusiano wa jamii balozi Rajab
Luhwavi amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia
Suluhu Hassan amefurahishwa na utulivu mkubwa walioonesha wananchi wa tarafa
hiyo na kusema serikali inafuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yake
yote katika eneo hilo.
Balozi
Luhwavi amewataka wananchi wa Endulen na Ngorongoro kwa ujumla kuendelea kuwa
wavumilivu wakati serikali katika ngazi mbalimbali ikiendelea kutekeleza
maelekezo ya Mheshimiwa Rais huku akisisitiza umuhimu wa wananchi hao kuendelea
kupendana na kushirikiana na serikali katika shughuli mbalimbali za maendeleo.
Kwa upande
wake Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ( NCAA) Dkt.
Elirehema Doriye amewaambia wananchi hao kuwa Mamlaka yake itasimamia na kutekeleza
maelekezo yote yanayoihusu mamlaka hiyo yaliyotolewa na wawakilishi wa
mheshimiwa Rais na kwamba hatua mbalimbali zimechukuliwa katika kutekeleza
maelekezo hayo ikiwa na pamoja na kuendeleza uhusiano wa NCAA na wananchi wa
Ngorongoro.
Kwa upande
wake mbunge wa Ngorongoro Mheshimiwa Emmanuel Ole Shangai ameipongeza serikali
kwa kuchukua hatua madhubuti za kuhakikisha miradi mbalimbali ya maendeleo
inatekelezwa na kusema kuwa ataendelea kusimamia suala hilo ili kuleta
maendeleo kwa wakazi wa eneo hilo.
Mheshimiwa
Ole Shangai amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt.
Samia Suluhu Hassan kutokana na upendo wake mkubwa kwa wananchi wa Tarafa ya
Ngorongoro uliopelekea wananchi wa eneo hilo kuruhusiwa kushiriki katika
uchaguzi wa serikali za mitaa baada ya kutolewa tangazo la kufuta vijiji katika tarafa hiyo.
Akizungumza
napema katika ibada hiyo Paroko wa kanisa katoliko Endulen Padri Albano
Mwombeki amewaongoza wananchi hao katika ibada hiyo ya shukranI na kuwataka
kuendelea kudumisha amani, utulivu na mshikamano ili waweze kujiletea maendeleo
yao na taifa kwa ujumla.
Na. Hamis Dambaya- NCAA
0 Maoni