Spika Mostaroine kuinadi Hifadhi ya Taifa Mikumi nchini Comoro

  

Spika wa Bunge la nchi ya Coromo, Mostaroine Abdou amevutiwa na vivutio mbalimbali vilivyomo ndani ya Hifadhi ya Taifa Mikumi ambapo ameahidi kuwa balozi wa kuvitangaza vivutio vyote alivyoviona pale ataporejea nchini kwake.

Mhe. Abdou aliyasema hayo jana Septemba 1, 2024 baada ya kutembelea vivutio adhimu vya utalii katika Hifadhi hiyo ambapo amesema kwamba amefurahishwa sana na wanyama kwani akiwa nchini kwake amekuwa akiwaona wanyama hao kwenye sinema pekee.

“Leo hii nimefika katika Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa ajili ya utalii,nimefurahishwa sana na wanyama ambao nimebahatika kuwaona napenda kuuhakikishia uongozi wa Hifadhi hii na Serikali ya Tanzania kwa ujumla kwamba nikirudi kwetu Comoro nitakuwa balozi wa kutangaza vivutio nilivyoviona,” alisema Abdou.

Mhe. Abdou pia, aliupongeza uongozi wa Hifadhi hiyo kwa kuhakikisha wanyama wote wanalindwa na kutunzwa dhidi ya wahalifu wakiwemo majangili ambapo alieleza kuwa kitendo cha kuwalinda wanyama hao Tanzania inanufaika zaidi kiuchumi kutokana na mapato yatokanayo na utalii.

Aidha, alitoa wito kwa jamii kufichua vitendo viovu vya ujangili na kuwasa wanaojihusisha na vitendo hivyo vya ujangili kuachana na tabia hiyo kwani vivutio ambavyo ameviona hususani wanyamapori kama vile Tembo, Nyani, Pundamilia, Swala, Viboko, Mamba na wengine wengi ni kwa sababu wanyama hao wanalindwa na kutunzwa vizuri.

“Nchi ya Comoro pamoja na Tanzania ni ndugu, tumekuwa marafiki wa muda mrefu na tumekuwa tukishirikiana katika masuala mbalimbali kwa maslahi mapana ya nchi hizi zote, hivyo na mimi pia nawaalika Watanzania kuja Comoro kutalii kwani ni nchi ya visiwa vingi hivyo mtajifunza kuogelea na kufuga samaki,” alisema Mhe. Abdou.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama, Mhe. Vita Kawawa (Mb) alisema anaushukuru uongozi wa Hifadhi hiyo kwani umeonesha ukarimu wa hali ya juu kwa Spika huyo ambapo anaamini ukarimu huo unatokana na misingi imara iliyojengwa na waasisi wa Taifa letu Tanzania.

Mhe. Kawawa alisema kuwa ziara ya Spika huyo katika hifadhi hiyo kutafungua fursa mbalimbali za kiuchumi kwani wananchi wengi wa Comoro watahamasika kwa wingi kuja kutalii katika hifadhi zilizopo hapa nchini hali ambayo itadumisha ushirikiano uliopo katika masuala ya kidiplomasia na kibiashara.

Kwa upande wake, Afisa Uhifadhi Mkuu, David Kadomo kwa niaba ya Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Mikumi, alisema uongozi wa hifadhi hiyo kwa kipekee kabisa una kila sababu ya kushukuru kupata ugeni huo mkubwa ambapo alisema kitendo cha Spika huyo kutembelea Hifadhi ya Taifa Mikumi utafungua fursa kwa wananchi wengine wa Taifa hilo kuja Tanzania kutalii.

Na Zainab Ally- Mikumi

Chapisha Maoni

0 Maoni